Majaliwa aaga Ruangwa baada ya miaka 15 ya ubunge
- Ni baada ya miaka 15 ya utumishi tangu alipochaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa mbunge wa Jimbo hilo mwaka 2010
Dar es salaam. Waziri Mkuu na Mbunge wa Jimbo la Ruangwa, Kassim Majaliwa, ametangaza rasmi kutoendelea kugombea ubunge wa jimbo hilo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.
Majaliwa amekuwa mbunge wa Ruangwa kwa miaka 15 mfululizo.
Akitangaza uamuzi huo leo Julai 2, 2025 mbele ya wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa na Wilaya ya Ruangwa, Majaliwa amewashukuru wananchi kwa kumuunga mkono tangu alipochaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa Mbunge wa Jimbo hilo mwaka 2010.
“Imefika wakati sasa wa kutoa nafasi kwa wengine walioko tayari kuendeleza kasi ya maendeleo. Tumejenga mshikamano, na kauli mbiu yetu ya ‘Ruangwa kwa Maendeleo Inawezekana’ iendelee kusonga mbele,” amesema Majaliwa.
Majaliwa ametoa wito kwa kamati hiyo kuwapa ushirikiano wagombea wote watakaojitokeza kwa nia ya kulitumikia jimbo hilo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Pia amewasihi wakazi wa Ruangwa kuendelea kushikamana hadi siku ya uchaguzi.
Katika hatua nyingine, Majaliwa amemshukuru Rais Samia pamoja na viongozi wa juu wa CCM kwa imani waliyoonyesha kwake kwa kipindi chote alichotumikia nafasi hiyo.
Itakumbukwa kuwa Juni 26, 2025 wakati akihitimisha kikao cha mwisho cha Bunge la 12, Majaliwa alitangaza kugombea tena nafasi ya ubunge wa Ruangwa.
Latest
