Maeneo sita ya kipaumbele bajeti Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
- Ni pamoja na kutambua, kuratibu na kuendeleza makundi maalum wakiwemo wafanyabiashara ndogondogo.
- Bajeti yapungua kwa asilimia nane, ya miradi ya maendeleo yapungua zaidi.
Dar es Salaam. Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Wanawake, Jinsia na Makundi Maalum imepanga kutekeleza vipaumbele sita kwa mwaka wa fedha 2024/25 ikiwemo kutambua, kuratibu na kuendeleza makundi maalum wakiwemo wafanyabiashara ndogondogo.
Waziri wa wizara hiyo Dorothy Gwajima aliyekuwa akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2024/25 leo Mei 17, 2024 bungeni Dodoma amesema, vipaumbele hivyo vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma za maendeleo na ustawi wa jamii.
“Kipaumbele cha kwanza ni kukuza ari ya jamii kushiriki katika kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo iliyoibuliwa ngazi ya msingi, Kuratibu afua za kukuza usawa wa kijinsia na kutokomeza vitendo vya ukatili, uwezeshaji wanawake kiuchumi, upatikanaji wa haki, ulinzi na malezi chanya ya watoto,”amesema Gwajima.
Vipaumbele vingine ni pamoja na kuratibu na kuimarisha utoaji wa huduma za msingi za ustawi wa jamii, kuboresha mazingira ya kufundisha na kujifunzia katika taasisi na vyuo vya ustawi na maendeleo ya jamii na kuimarisha ushiriki na mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO) katika maendeleo ya Taifa.
Katika kutekeleza vipaumbele vilivyoainishwa, wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2024/25 imeomba Bunge liliridhie matumizi ya Sh67.9 bilioni ambapo kati ya fedha hizo Sh47.5 bilioni ni fedha za matumizi ya kawaida na Sh20.4 bilioni ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Hata hivyo, fedha hiyo imepungua kwa zaidi ya Sh 7 bilioni kutoka Sh74 bilioni iliyoidhinishwa mwaka 2023/24.
Kwa upande wa fedha zilizoombwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo zimepungua kwa asilimia 49.7 sawa na Sh10.1 bilioni kutoka Sh30.6 iliyoidhinishwa kwa mwaka wa fedha 2023/24.
Aidha, Gwajima ametaja maeneo ambayo yametengewa fedha kwa mwaka 2024/25 ikiwemo utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu kwa wafanyabiashara ndogondogo Sh10.5 bilioni ili kuongeza mitaji na kuboresha shughuli zao za kiuchumi ingawa fedha iliyotengwa na kuidhinishwa kwa ajili ya jambo hilo mwaka 2023/24 haikutolewa.
Latest



