Madhara ya corona: UNICEF yaangazia namna ya kuwarudisha wanafunzi shuleni
- Imesema wanafunzi waliopo vijijini hawapati fursa ya kujifunza.
- Yaandaa mwongozo utakaotumika kuwarudisha wanafunzi shuleni.
Dar es Salaam. Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) limeeleza kuwa linaangalia uwezekano wa kufungua shule katika nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika ambako wanafunzi wengi hawapati fursa ya kusoma kutokana na janga la Corona.
Janga hilo limewaathiri zaidi watoto waishio vijijini ambao wanakabiliwa na changamoto ya kukosa umeme na intaneti, licha ya Serikali za nchi hizo kuanzisha utaratibu wa kusoma kwa njia ya redio na mtandaoni.
UNICEF katika taarifa yake iliyotolewa Mei 4 nchini Kenya na Afrika Kusini, imeeleza kuwa zaidi ya watoto milioni 127 wa shule za awali, msingi na sekondari katika nchi hizo wataendelea kukaa nyumbani kutokana na kutotengamaa kwa hali ya virusi vya COVID-19.
“Katika maeneo mengi ya dunia, kujifunzia nyumbani kumesaidiwa na zana za mtandaoni. Hata hivyo, katika maeneo ya Afrika Mashariki na Kusini, kupenya au kusambaa kwa intaneti ni kugumu, ambapo ni kaya moja tu kati ya tano sawa na asilimia 22 ambao wana intaneti, wakati asilimia 84 ya watu wa vijijini ambako idadi kubwa ya wanafunzi wanapatikana, hawana umeme,” imeeleza taarifa hiyo.
Katika Kushughulikia sintofahamu hiyo, UNICEF imetangaza usaidizi zaidi kwa janga hili la elimu ambalo halijawahi kutokea, wakati ikiendelea kutafuta namna ya ufunguzi wa shule unaozingatia mwongozo wa usalama.
Zinazohusiana
- Kanda ya ziwa yatikisa matokeo darasa la saba 2019
- Halmashauri zilizoshika mkia matokeo darasa la saba 2019
- Mara itatoboa katika mtihani wa darasa saba 2019?
UNICEF imeandaa mwongozo mpya wa kiufundi uliopewa jina “Mfumo wa kufungua Shule” ambao unatoa muundo wa kufungua upya shule ili kuwapa fursa ya kusoma wanafunzi ambao hawawezi kujifunza kwa njia ya mtandao au redio.
Mwongozo huo uliandaliwa kwa ushirikiano wa Shirika la Mpango wa Chakula (WFP), Benki ya Dunia, Shirika la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO na UNICEF yenyewe.
Hata hivyo, haijaweka bayana ni lini wanatarajia mpango huo utaanza kutekelezwa.
Mpaka sasa shirika hilo limezisaidia Serikali za nchi hizo zaidi ya dola milioni 5.4 (Sh12.5 bilioni) kwa ajili ya masomo na pia kwa ajili ya maandalizi ya kuzifungua shule huku ufadhili zaidi ukiwa katika mipango.
Latest