Lhrc yataka wanawake waongezewe nguvu za kisheria, kidijitali
- Yawafikia wanawake 300 wa Bagamoyo.
- Wapewa mafunzo ya kutumia fursa za kidijitali na kisheria.
- Yawataka wanawake kuamka na kupigania haki zao.
Dar es Salaam. Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimewajengea uwezo na kuwapa msaada wa kisheria wanawake zaidi ya 300 wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.
Maadhimisho hayo yaliyofanyika leo March 2, 2023 kwenye viwanja vya Mwakalenge Bagamoyo, yamefungua fursa mpya kwa wanawake wa Mkoa wa Pwani kwenye masuala mbalimbali ikiwemo teknolojia na ubunifu yanayotajwa kuchangia maendeleo kwa kiasi kikubwa.
Mkurugenzi wa Lhrc, Anna Henga aliyekuwa akizungumza katika maadhimisho hayo amesema uwezeshwaji huo utawakomboa wanawake ambao hushindwa kupata nafasi ya mafunzo na uelewa wa masuala yanayoendelea katika jamii kutokana na mlundikano wa shughuli nyingi za nyumbani.
“Mafunzo ya teknolojia na ubunifu yatawapa wanawake fursa za kujiendeleza na kuchangia maendeleo ya jamii zao kwa ujumla hivyo kuna haja ya kuendelea kushirikisha wanawake, kuamini wanawake pamoja na kuhakikisha wanapata mafunzo juu ya teknolojia pamoja na digiti,” amesema Wakili Henga.
Soma zaidi
Uwezeshwaji huo utawasaidia wanawake katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikwemo kuongeza ubunifu kwenye biashara pamoja na kuongeza usawa wa kijinsia katika matumizi ya teknolojia na vifaa vya kiteknolojia.
“Ni matumaini ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kuwa elimu hii wataifikisha kwa wengine na wataitumia ipasavyo kuweza kujiendeleza wao wenyewe,” amesema Henga.
Mbali na mafunzo hayo, Lhrc pia imetoa msaada kwa wanawake wenye changamoto za kisheria ili waweze kutambua haki zao na kupata msaada.
Kila Machi 8, dunia husheherekea siku ya wanawake duniani na kwa mwaka huu kaulimbiu ya siku hiyo inasema “Ubunifu na mabadiliko ya teknolojia; chachu kuleta usawa wa kijinsia”.
Maadhimisho haya yanakuja wakati dunia ikiwa katikati ya maendeleo ya teknolojia na kidigitali ambayo kwa kiasi kikubwa yamewaacha wanawake.
Serikali toeni mafunzo ya teknolojia kwa wanawake
Lhrc, imetumia maadhimisho hayo kutoa wito kwa Serikali kuendelea kuwapa wanawake nafasi za mafunzo ya teknolojia, dijiti, masoko pamoja na kutunga sheria mahsusi za kupambana na vitendo vya ukatili dhidi yao.
“Toeni elimu kwa jamii kuhusu usawa wa kijinsia na haki za wanawake na kuweka programu maalumu za kusaidia wanawake wa vijijini kutumia teknolojia na upatikanaji wa huduma za kiteknolojia katika maeneo yao,” ameongeza Henga.
Sambamba na hayo wanawake wametakiwa kujiamini na kutumia fursa mbalimbali ikiwemo teknolojia na digitali zenye uwezo wa kuboresha maisha yao.
Latest
