Kusaya: Udhibiti sumukuvu kuongeza uzalishaji chakula Tanzania
- Kudhibiti tatizo la sumukuvu ili kuboresha afya ya jamii kwa kuhakikisha Taifa linazalisha na kuuza chakula salama kwa walaji.
- Kuna aina 400 za sumu hiyo lakini yenye madhara makubwa ni ya “Aflatoxin” ambayo hukutwa katika nafaka aina ya mahindi na karanga.
Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya amewataka wadau wa usalama wa chakula kuisaidia Serikali kutekeleza mradi wa miaka mitano wenye lengo la kudhibiti tatizo la sumukuvu ili kuboresha afya ya jamii kwa kuhakikisha Taifa linazalisha na kuuza chakula salama kwa walaji.
Ikiwa sumukuvu hiyo itadhibitiwa itasaidia uzalishaji wa mazao ya chakula yenye viwango vya ubora vinavyotakiwa kitaifa na kimataifa.
“Kutokana na changamoto ya sumukuvu hapa nchini kwetu ambapo kwa taarifa nilizopata ni kuwa tatizo hili limekuwa likijirudia rudia kwa miaka mitatu mfululizo 2016, 2017, 2018 na 2019, utekeleaji wa mradi huu ni muhimu sana na hivyo nataka kila mmoja awajibike na sio wizara ya Kilimo pekee” amesema Kulaya.
Kusaya alikuwa akizungumza wakati akifungua kikao cha pili cha kamati ya kusimamia mradi wa kudhibiti sumukuvu nchini (TANIPAC) kilichofanyika leo mkoani Morogoro.
Kusaya amesema usalama wa chakula Tanzania unategemea kilimo kwa kiasi kikubwa, na kuongeza kuwa “tunalo jukumu kubwa la kuhakikisha kwamba tunaendelea kukipa kilimo uzito unaostahili kwa kukabiliana na changamoto zinazojitokeza wakati wowote.”
Kwa mujibu wa Wizara ya Kilimo, Sekta ya kilimo inaajiri asilimia 65 ya nguvukazi na inachangia asilimia 30 ya pato la Taifa (GDP), huku ikichangia takriban asilimia 65 ya malighafi za viwandani na takribani asilimia 100 ya chakula kinachotumika ndani ya nchi.
Zinazohusiana
- Apps 10 za kilimo zinazoweza kuwanufaisha wakulima Tanzania
- Wakulima washauriwa kutumia teknolojia ya kisasa ya kilimo cha umwagiliaji
- PASS kuwawezesha vijana sekta ya kilimobiashara
Naye Mtaalamu wa Shirika la viwango Tanzania (TBS), Dk Analyse Camara amesema tatizo la sumukuvu ni kubwa duniani na kwamba mtu anapotumia kiwango kikubwa cha sumu hiyo maisha yake yanakuwa hatarini, kufa au kwa watoto kudumaa.
Amesema uwepo wa sumukuvu ulitambulika duniani kwa takribani miaka 600 kabla ya kuzaliwa Kristo na kujulikana chanzo chake mwaka 1960 watu walipobaini uwapo wa sumu hiyo na athari zake kwa binadamu.
Amesema kuna sumukuvu aina 400 lakini yenye madhara makubwa ni ya “Aflatoxin” ambayo hukutwa katika nafaka aina ya mahindi na karanga.
Mradi wa TANIPAC una thamani ya dola za Marekani milioni 33.3 unajikita katika ujenzi wa miundombinu muhimu kama vile ujenzi wa maghala, uanzishwaji wa maabara kuu ya kilimo, kituo mahiri cha Usimamizi wa mazao ya Nafaka (“Postharvest Centre of Excellence for Grains”) na uimarishaji wa miundombinu ya kituo cha utafiti wa magonjwa ya Kabailojia kilichopo Kibaha mkoani Pwani.
Latest
