Kanzidata ya wavuvi yaanzishwa, kukopesheka taasisi za fedha

February 7, 2020 7:41 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Waziri Mpina asema itawasaidia wavuvi wa Tanzania kuaminika na kukopesheka katika benki mbalimbali.
  • Itakuwa pia ni fursa ya kupata mitaji ya kuendesha shughuli zao na kipato cha familia. 
  • Serikali yaangalia uwezekano wa kuwapatia bima. 

Dar es Salaam. Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesema kanzidata ya uvuvi (uvuvi database) iliyoanzishwa na wizara yake itawasaidia wavuvi wa Tanzania kuaminika na kukopesheka katika benki mbalimbali ili kupata mitaji ya kuendesha shughuli zao na kipato cha familia. 

Mpina aliyekuwa akizungumza Bungeni jijini Dodoma leo (Februari 7, 2020) amesema wavuvi wengi walikuwa hawaamiki wala kuheshimiwa kwa sababu ya shughuli zao za kuhamahama.

Amesema kanzidata hiyo yenye taarifa muhimu za wavuvi na maeneo waliko inaweza kuwa mkombozi wa kuboresha maisha yao.

“Wizara ya Uvuvi imeandaa uvuvi database (kanzidata) ambacho kilikuwa kipengele kigumu sana ambacho kilikuwa kinawafanya wavuvi wetu wasiaminike kwenye mabenki kwa sababu ya shughuli zao za kuhamahama.

“Kila mtu mwenye benki anakuwa na mashaka kuwa fedha zake anakozipeleka. Sasa tulipoanzisha uvuvi database, sasa hivi benki yoyote ile ikitaka kumkopesha mvuvi ambaye yuko Buchosa, Ukerewe, Mafia ambaye yuko maeneo mengine watamuona na kazi zake anazozifanya,” amesema Mpina. 

Amesema hatua hizo zilizochukuliwa na wizara yake zinaenda kuongeza imani kubwa kwa wavuvi na dhana kwamba wavuvi hawakopesheki sasa itakuwa mwisho.


Zinazohusiana:


Waziri huyo alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya aliyetaka kujua mkakati wa Serikali kuwawezesha wavuvi waliojiajiri kupata mitaji kuendesha shughuli zao kwa vifaa vya kisasa. 

Awali, Naibu Waziri Abdallah Ulega amesema zipo sababu mbili ambazo zinawafanya wavuvi wasikopesheke ni kukosa dhamana na bima ya shughuli wanazofanya.

Hata hivyo, amesema wanaendelea kuzungumza na benki kuwasaidia wavuvi ambapo benki ya Posta (TPB) tayari imeanzisha akaunti maalum kwa ajili ya wavuvi na wafugaji ambayo inawawezesha kupata mikopo. 

Pia wamelishawishi Shirika la bima la Taifa (NIC) kusaini mkataba maalum na wavuvi ili kuwapatiwa bima zitakazowahakikishia usalama wa kazi zao.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW