Instagram yatozwa faini ya bilioni 940 uvunjanji faragha za watoto
- Adhabu inafuatia uchunguzi kuhusu mpangilio wa Instagram ambao unaruhusu watoto kufungua akaunti zilizoonyesha maelezo ya mawasiliano.
Dar es salaam. Mtandao wa kijamii wa Instagram umetozwa faini ya Euro 405 milioni sawa na Sh940 bilioni kwa kutolinda taarifa za faragha za watoto wanaotumia mtandao huo kwa kuonyesha vitu vilivyozuiliwa kwa kundi hilo.
Kwa mujibu wa Kanuni ya Jumla ya Ulinzi wa Data ya Umoja wa Ulaya (GDPR), hilo ni kosa kwa sababu watoto wanahatarisha usalama wa watoto wanapoumia mtandao huo unaokuwa kwa kasi.
Adhabu ya faini hiyo ilitolewa Septemba 5, 2022 na Tume ya Kulinda Data ya Ireland (DPC) kutokana na jinsi Instagram inavyoshughulikia mipangilio ya faragha ya watoto kwenye programu yake.
Hatua hiyo imefikiwa baada ya uchunguzi ulioangalia uchakataji wa taarifa za watoto, ambapo taarifa kama vile anwani za barua pepe na nambari za simu huonekana wazi.
Pia ilichunguza jinsi baadhi ya akaunti za watoto zilivyowekwa hadharani kama chaguo la msingi, badala ya faragha.
Hata hivo, msemaji wa Meta Bw Andy stone, kampuni mama ya Instagram amesema wamefanya marekibisho ya usalama wa watoto tangu mwaka jana na kwamba uchunguzi wa sasa umelenga mipangilio ya zamani.
“Mtu yeyote aliye na umri wa chini ya miaka 18 anaweka akaunti yake kuwa ya faragha kiotomatiki anapojiunga na Instagram, kwa hivyo ni watu wanaojua tu wanaoweza kuona anachochapisha, na watu wazima hawawezi kutuma ujumbe kwa vijana ambao hawawafuati.
“Tulishirikiana kikamilifu na DPC wakati wote wa uchunguzi wao, na tunakagua kwa uangalifu uamuzi wao wa mwisho,” alisema msemaji huyo.
Uamuzi unaozingatia watoto unagusa eneo nyeti kwa kampuni za mitandao ya kijamii, na kuilazimu kushughulikia taarifa za watoto kwenye huduma zao.
Soma zaidi
Instagram ilikabiliwa na ukosoaji na uchunguzi baada ya Jarida la Wall Street kuchapisha nakala zinazoonyesha kwamba utafiti wa ndani wa kampuni hiyo uligundua kuwa Instagram ilikuwa hatari kwa wasichana wadogo wenye wasiwasi wa taswira ya mwili.
Faini ya Instagram inafikia asilimia 1 ya mapato halisi ya Meta kwa 2021, na kuashiria maamuzi ya faragha ya Umoja wa Ulaya yenye uwezo mkubwa wa kulazimisha mabadiliko ya mbinu za kukusanya data na makampuni mengi makubwa ya teknolojia ikiwa yatathibitishwa katika uwezekano wa kukata rufaa mahakamani.
Udhibiti huu unaweza ukabadili taswira ya sekta pana za utangazaji wa dijitali na mitandao ya kijamii.
Kesi nyingine inayoongozwa na Ireland inaweza kuamuru Facebook kusitisha kutuma data kuhusu watumiaji wake kwenye seva za zake za Marekani.
Meta imesema katika faili la kesi hiyo kuwa ikiwa uamuzi huo utatekelezwa kabla ya Umoja wa Ulaya na Marekani kuandaa njia mpya ya kisheria ya uhamisho huo wa data, inaweza kusimamisha baadhi ya huduma zake barani Ulaya.
Latest