Hii ndiyo maana ya Nchimbi ‘kufukuzwa’ uanachama CCM
- Kwa mujibu wa katiba ya CCM ya mwaka 1977, Toleo la Desemba 2022 kuna tofauti kati ya kufutwa uanachama na kufukuzwa uanachama.
Dar es Salaam. Jana Agosti 26, 2026, Chama cha Mapinduzi (CCM), kilitangaza kumfukuza uanachama Dk Emmanuel Nchimbi alietangaza kujiudhuru kutoka kwenye nafasi ya Makamu wa Rais na kuachia madaraka yake ifikapo Septemba 4, 2026.
Katibu Mkuu wa CCM, Dk Asha-Rose Migiro aliwaambia waandishi wa habari kuwa Nchimbi amefukuzwa kutoka ndani ya CCM kutokana na madai ya kukiuka Katiba, kanuni na taratibu za Chama.
Kwa mujibu wa katiba ya CCM ya mwaka 1977, Toleo la Desemba 2022, uanachama wa CCM unaweza kukoma kwa sababu sita.
Sababu hizo ni pamoja na kufariki, kujiuzulu kwa hiari, kujiunga na chama kingine cha siasa, kutotimiza masharti ya uanachama, kufutwa uanachama kwa mujibu wa katiba ya chama pamoja na kufukuzwa uanachama.
Unachotakiwa kufahamu ni kuwa kuna tofauti kati ya kufutwa na kufukuzwa uanachama kwa mujibu wa katiba ya CCM.
Wakili William Maduhu kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) anasema kuachishwa uanachama kunaweza kutokea pale mwanachama anaposhindwa kutimiza masharti ya uanachama kwa mujibu wa Katiba ya Chama, ikiwemo kutokuwa mwanachama hai.
Tofauti na kuachishwa uanachama, kufukuzwa kutoka kwenye chama kunahusisha hatua za kinidhamu zinazochukuliwa kwa mujibu wa Katiba na taratibu za chama, pale mwanachama anapokiuka miiko, maadili au kanuni za chama.
Katika mchakato huo, mwanachama hupewa fursa ya kusikilizwa, kujieleza na kujitetea, na endapo atabainika kuwa amekiuka masharti yanayohusika, hatua ya kumfukuza uanachama inaweza kuchukuliwa.
“Kufukuzwa ni kwamba kunakuwa kuna mchakato umefuatwa, umeandikiwa barua, umesikilizwa, umejitetea, vikao vimekaa vimekuita lakini vikagundua kuwa hukuwa na mashiko wanakufukuza,” amesema Wakili Maduhu.
Hivyo kwa mujibu wa taarifa ya Dk Migiro, Dk Nchimbi amefukuzwa uanachama, jambo litakalomuweka nje ya shughuli zote za kiuanachama ndani ya CCM kwa sasa.