Hawa hapa wagombea 10 wa viti maalum UVCCM
- Ng’wasi Kamani aongoza kwa kura nyingi kati ya wagombea 31 wa Tanzania Bara.
- Latifa Juakali na Mwenezi Suluhu waibuka vinara upande wa Zanzibar.
Dar es Salaam. Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza matokeo rasmi ya uchaguzi wa viti maalum kupitia Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), uliofanyika jijini Dodoma Agosti mosi mwaka huu.
Miongoni mwa walioibuka washindi ni pamoja na Jesca Magufuli, mtoto wa Rais wa Serikali ya awamu ya tano, hayati John Magufuli, Ng’wasi Kamani na Halima Bulembo.
Uchaguzi huo ulihusisha jumla ya wagombea 48, ambapo 31 kati yao ni kutoka Tanzania Bara na 17 kutoka Zanzibar.
Msimamizi wa uchaguzi huo Mohamed Abood ametangaza matokeo rasmi asubuhi ya leo, Agosti 2, 2025 baada ya kuhesabu kura zilizopigwa usiku wa kuamkia siku hiyo.
Uchaguzi huo pia ulihusisha nafasi mbili za uwakilishi katika Baraza la Wawakilishi Zanzibar kupitia kundi la vijana.

Kwa upande wa Tanzania Bara, jumla ya kura zilizopigwa zilikuwa 2,466, ambapo kura halali zilikuwa 2,454 na zilizoharibika zilikuwa 12.
Katika uchaguzi huo, wagombea sita walioshinda nafasi za viti maalum kupitia kundi la vijana ni Ng’wasi Kamani aliyepata kura 409, Jesca Magufuli kura 391, Halima Bulembo kura 320, Lulu Mwacha kura 316, Juliana Masaburi kura 282 na Timida Mpoki kura 280.
Kwa upande wa Zanzibar, jumla ya kura zilizopigwa zilikuwa 1,652, ambapo kura halali zilikuwa 1,644 na zilizoharibika nane.
Washindi wanne waliopata kura nyingi zaidi kati ya wagombea 17 ni Latifa Juakali aliyepata kura 357, Mwenezi Suluhu kura 339, Zainabu Issa kura 334, na Ashina Mzee aliyepata kura 151.

Kwa upande wa nafasi za uwakilishi kupitia Baraza la Wawakilishi Zanzibar, jumla ya kura zilizopigwa zilikuwa 822, ambapo kura halali zilikuwa 818 na zilizoharibika nne.
Washindi wa nafasi hizo mbili ni Salha Mwinjuma aliyepata kura 255 na Hudhaima Tail aliyepata kura 235.
Uchaguzi huo ulitanguliwa na Mkutano Mkuu Maalum wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) uliohusisha wajumbe kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Ikiwa majina yao yataridhiwa na Kamati Kuu ya CCM basi watakuwa wabunge katika Bunge lijalo.