Hautahitaji tena “password” kutumia iPhone kuanzia Oktoba
- Apple itaondoa kipengele hicho kuimarisha usalama wa watumiaji wake.
- Badala yake watumiaji watatumia alama za vidole na utambuzi wa uso.
Kama ni mmoja wa watumiaji wa simu aina ya iPhone na haupendi kutumia nenosiri (password) katika simu yako, basi huenda maombi yako yamejibiwa.
Kampuni ya Apple imesema inaratjia kuingiza sokoni simu mpya za iPhone mapema Oktoba mwaka huu ambazo hazitakuwa na kipengele cha nenosiri.
Badala yake simu hizo zitakuwa na machaguo mawili yatakayomuwezesha mtu kuingia au kuilinda simu yake kwa alama za vidole (finger print) na utambuzi wa uso (facial recognition).
Kurt Knight, Mkurugenzi Mkuu wa Masoko wa Apple akiwa California nchini Marekani Agosti 4, 2022 alieleza kuwa hatua hiyo imekuja ili kuimarisha usalama wa wateja wao wakati wanatumia simu za iPhone kwa sababu nenosiri imekuwa miongoni mwa milango ya wadukuzi.
“Password ni muhimu kwa usalama wa taarifa na fedha, lakini pia ni mojawapo ya udhaifu wa kiusalama ambao watumiaji wanakabiliana nao leo,” alisema Knight.
Tangazo

Mabadiliko hayo pia yatawanufaisha watumiaji wa kompyuta za Mac ambapo kwa wanaweza kuingia kwa kutumia utambuzi wa uso au alama za vidole.
Mabadiliko yatapatikana kwenye mfumo endeshi mpya (iOS16) kwa iPhone pamoja na mfumo endeshi wa X (OSX) wa Mac.
“Uthibitishaji wa kitambulisho cha uso na kitambulisho cha kugusa kwa kidole hukupa urahisi na bayometriki tunazoweza kufikia kwa kutumia iPhone. Sio lazima kununua kifaa kingine, lakini pia sio lazima ujifunze tabia mpya,” Darin Adler, mmoja wa maafisa wa Apple alieleza umuhimu wa mabadiliko hayo.
Mabadiliko hayo ya Apple siyo ya kwanza, mwaka jana kampuni ya Microsoft nayo iliachana na matumizi ya nenosiri ili kuimarisha mifumo ya vifaa vyake vya kielekroniki na programu.
Latest
