Halmashauri ya mji wa Mbulu inavyokimbiza ukusanyaji wa mapato
- Yashika nafasi ya kwanza kwa kuvuka lengo la ukusanyaji.
- Ilikuwa inashika nafasi ya mwisho kwa miaka mitatu.
- Serikali yazionya halmashauri zinazosuasua ukusanyaji mapato.
Dar es Salaam. Unaweza kusema wamefuta aibu ya miaka iliyodumu kwa miaka mitatu baada ya Halmashauri ya Mji wa Mbulu kushika nafasi ya kwanza katika ukusanyaji wa mapato ya ndani.
Halmashauri hiyo iliyopo mkoani Manyara imeshika nafasi ya kwanza kati ya halmashauri za miji 21 zilizopo Tanzania.
Siyo kwa sababu imekusanya mapato mengi kwa mwaka wa fedha wa 2021/22 bali ni kwa sababu imevuka lengo la makisio iliyojiwekea awali.
Kwa mujibu wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Innocent Bashungwa, katika mwaka wa fedha uliopita Mbulu ilikusanya Sh1.4 bilioni.
Bashungwa katika taarifa ya Tamisemi kuhusu mapato na matumizi ya mapato ya ndani ya halmashauri kwa mwaka wa fedha 2021/2022 amesema halmashauri hiyo imekusanya zaidi ya makadirio yaliyowekwa awali kwa asilimia 140.
Halmashauri hiyo iliyokusanya Sh1.4 bilioni iliweka makadirio ya kukusanya Sh1 bilioni kwa kipindi cha Julai 2021 hadi June 30, 2022.
“Halmashauri ya Mji wa Mbulu imeongeza ufanisi kwani kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo imekuwa ikishika nafasi ya mwisho, alisema Waziri Bashungwa.
Halmashauri ya Mji wa Mafinga iliyokusanya Sh6.3 bilioni imeshika nafasi ya pili kwa kufanya vizuri katika kukusanya mapato.
Mapato hayo ni sawa na ongezeko la asilimia 28.6 la makadirio ya mapato ya Sh4,9 bilioni yalitarajiwa kukusanywa mwaka wa fedha uliopita.
Soma zaidi:
Nafasi ya tatu imeshikiliwa na Halmashauri ya Mji wa Ifakara mkoani Morogoro ambayo ilikusanya Sh4.8 bilioni. Makusanyo hayo ni sawa na ongezeko la asilimia 24.7 ya makadirio ya Sh3.9 bilioni yaliyokusudiwa awali.
Halmashauri za miji mingine zilizoingia kwenye orodha ya tano bora ni pamoja na Halmashauri ya Mji wa Tunduma iliyokusanya jumla ya Sh8.7 bilioni, Mbinga (Sh2.1 bilioni) na Newala iliyokusanya Sh2.3 bilioni.
Fedha hizo za makusanyo ya halmashauri hutumika katika shughuli mbalimbali za kuboresha miundombinu na huduma za kijamii ikiwemo shule, hospitali na maji kwa usaidizi wa Serikali Kuu.
Halmashauri za miji zilizoshika mikia
“Halmashauri ya Mji wa Nanyumbu imekuwa ya mwisho kwa kukusanya asilimia 71 ya makisio ya mwaka ikifuatiwa na Halmashauri za Mji wa Korogwe asilimia 84 na Halmashauri ya Mji wa Geita asilimia 88,” alisema Bashungwa
Mji wa Nanyumbu uliopo mkoani Mtwara uliojiwekea makadirio ya Sh2 bilioni umeishia kukusanya Sh1.4 bilioni hali iliyofanya ushike mkia kwenye orodha ya ukusanyaji wa mapato.
Mji wa Korogwe uliweka makisio ya kukusanya Sh2 bilioni ulikusanya Sh1.8 bilioni kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Sambamba na hilo, Halmashauri ya Mji wa Geita iliyojiwekea makisio ya kukusanya Sh10 bilioni imekusanya Sh9 bilioni na kuufanya ishike nafasi ya tatu kutoka mwisho.
Wizara yaanza kuchukua hatua
Kutokana na tathmini hiyo, Tamisemi imeanza kuchukua hatua kama kuwabadilisha vituo baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo.
Hatua nyingine ni kufanya msawazo kwa watumishi na kuwabadilishia majukumu baadhi ya wakuu wa idara na vitengo kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi na kuondoa utendaji kazi wa mazoea.