Elimu ya bima itakavyopunguza ajali za barabarani
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akikagua mchoro wa mfano wa barabara wakati alipotembelea mabanda katika Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani. Picha | Mariam John.
- Inasaidia vyombo vya moto kuwa na ubora unaotakiwa.
Mwanza. Mamlaka ya Bima Tanzania (TIRA) ifikapo mwaka 2030 inatarajia kuwa itakuwa imewafikia Watanzania kwa zaidi ya asilimia 80 kwa kuwapatia uelewa wa matumizi ya bima itakayosaidia kupunguza ajali za barabarani.
Kamishna wa TIRA, Khadija Said akizungumza na Nukta Habari (www.nukta.co.tz) amesema jukumu kubwa walilonalo kwa sasa ni kuongeza uelewa kwa Watanzania waliofikia miaka 18 wajue umuhimu wa kukata bima za vyombo vya moto ambavyo hivi sasa vinagharimu maisha ya watu.
Mamlaka hiyo ina mikakati mbalimbali itakayosaidia kupunguza tatizo hilo nchini ikiwemo kufanya kazi kwa karibu na Jeshi la Polisi kufanya doria kudhibiti ajali za barabarani.
“Pia tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi ambapo katika maadhimisho ya siku mwanamke duniani takribani watu 300 walipata elimu ya umuhimu wa bima kwenye vyombo vya moto,” amesema Said.
Madereva bado kuhusu bima
Amesema baadhi ya wamiliki wanakataa kukata bima za vyombo vyao vya moto wakidai hawanufaiki ipasavyo ikiwemo muda wanaokata ni mfupi.
“Kwa maana kwamba iwapo Tira wanakata bima kwa miezi saba wao wakate kwa miezi sita jambo ambalo sio nzuri,” amesema Said.
Afisa Uhusiano wa TIRA, Oyuke Faustine ameitaja bima kuwa ni moja ya nguzo za kukinga ajali kwakuwa abiria anaweza kutumia mfumo uliowekwa na mamlaka hiyo kuhakiki chombo anachopanda iwapo kimekatiwa bima.
Ameitaja mifumo hiyo kuwa ni pamoja na kutumia tovuti ya TIRA au kuingia kwenye menyu ya M-Pesa kwa kubonyeza *152*00#.
Mwenyekiti wa Chama cha Shule Binafsi cha Udereva (Chaushubuta) amesema pamoja na suala la utoaji wa bima kwenye vyombo vya moto lakini pia amevitaka vyuo vya udereva kutochukia ukaguzi unaofanywa na Jeshi la Polisi katika shule zao kwa kuwa haulengi kuzifungia bali kuzifanyia maboresho.
Amesema kwa kufanya hivyo shule za udereva zitaweza kutoa elimu bora itakayosaidia kupunguza ajali za barabarani.
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Camilius Wambura ametoa maagizo ya kufanyika kwa ukaguzi kwenye vyuo vinavyotoa mafunzo ya udereva ili kujiridhisha kama bado vina uwezo wa kutoa elimu hiyo na viwango vya walimu wanaotoa elimu na mitaala ya udereva.
“Tumebaini kuwepo kwa baadhi ya vyuo vya udereva kukosa sifa na weledi na kutumika kama madaraja ya vyeti feki na wasajili wa madereva kutoa leseni bila kufuata taratibu,” amesema Wambura.
Latest