Bajeti ya Serikali Tanzania yapaa hadi Sh62.33 trilioni
- Sehemu kubwa ya bajeti itatumika katika matumizi ya kawaida.
- Misaada klutoko nje yatarajiwa kupungua kwa asilimia asilimia 39.1
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania inapanga kukusanya na kutumia Sh62.33 trilioni katika mwaka wa fedha 2026/27 ikiwa ni ongezeko la zaidi ya Sh5.84. trilioni ndani ya mwaka mmoja huku sehemu kubwa ikitarajiwa kutumika katika matumizi.
Kiwango hicho cha bajeti ni sawa na ongezeko la asilimia 10.3 kutoka Sh56.49 trilioni iliyoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya mwaka wa fedha 2025/26 unaohitimishwa Juni mwaka huu.
Matarajio ya bajeti hiyo ya Serikali yanalingana na kiwango cha Sh62.33 bilioni kilichowasilishwa Machi mwaka huu wakati wa uwasilishaji wa mapendekezo ya mfumo na ukomo wa bajeti ya Serikali kwa mwaka fedha wa 2026/27.
Hii ni bajeti ya kwanza itakayotekelezwa ndani ya Dira ya Taifa 2050 ambayo pamoja na mambo mengine imelenga kuufikia uchumi wa Sh1.8 ‘quadrillion’ (Dola za Marekani trilioni moja).
Kupitishwa kwa bajeti hiyo kutafungua ukurasa wa kwanza wa utelezaji wa maono mengine ya dira hiyo ikiwemo kukuza uchumi endelevu na jumuishi wa kipato cha kati cha juu utakaowawezesha Watanzania kuingiza Sh12.5 milioni na Sh20.8 milioni.
Mapato ya ndani kupaa, misaada ikipungua
Serikali ya Tanzania imeeleza dhamira yake ya kuongeza nguvu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, hasa kutokana na matarajio ya kupungua kwa misaada kutoka nje.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Omar, amesema kwamba katika mwaka wa fedha unaoanza Julai 2026, Serikali inatarajia kukusanya mapato ya ndani ya Sh46.79 trilioni.
“Mapato ya kodi ni Sh36.99 trilioni, mapato mengine ni Sh9.24 trilioni (ikijumuisha mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Sh1.97trilioni) na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo Sh563.1 bilioni,” amesema.
Kwa mujibu Balozi Omar misaada kutoka kwa kwa washirika wa maendeleo inatarajiwa kupungua kwa asilimia 39.1 kwa mwaka 2026/27. Ikichangiwa na kubadilika kwa sera za baadhi ya washirika wa maendeleo akiwataka wananchi kuwajibika kulijenga Taifa.
“Tanzania ni Taifa letu na sisi ndio wenye wajibu wa kulijenga. Ni wajibu wa wananchi wote kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kulipa kodi kwa hiari, na kushikamana na Serikali katika kuleta maendeleo,” amesema
Pamoja na hayo, Sh10.12 trilioni itatumika kulipa stahiki za watumishi na michango ya pensheni (Serikali Kuu) huku Sh6.32 trilioni ikighramia michango ya hifadhi za jamii.