Bugando yazindua maabara kupima Uviko-19, majibu kutoka ndani saa 24

November 10, 2021 5:12 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Sampuli hazitatumwa katika maabara ya Taifa jijini Dar es Salaam.
  • Itapunguza muda wa kupata majibu ya Uviko-19 hadi saa 24 kutoka saa 72.
  • Maabara hiyo pia  itapima magonjwa ya saratani, homa ya ini, kifua kikuu, virusi vya Ukimwi (VVU) na vinasaba.

Mwanza. Wakazi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa ambao walikuwa wanasubiri kupata majibu ya kipimo cha Uviko-19 kwa saa 72, sasa wana kila sababu ya kutabasamu kwa kuwa wataweza kupata majibu hayo ndani ya saa 24 baada ya huduma za vipimo kusogezwa karibu.

Serikali ya Marekani imefanikisha kukarabati na ununuzi wa vifaa vya maabara ya kisasa katika ya Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando ya jijini Mwanza itakayokuwa na uwezo wa kupima virusi vya Uviko-19  badala ya kutuma vipimo hivyo katika maabara ya Taifa iliyopo jijini Dar es Salaam.

Zaidi  ya Sh36 bilioni zimetumika kuboresha maabara hiyo ambayo pia inajihusisha na matibabu kwa wenye virusi vya Ukimwi  pamoja na maeneo mengine muhimu katika utoaji wa huduma za afya.

Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Dk Fabian Massaga amesema licha ya maabara hiyo  kupima Uviko-19, pia itapima magonjwa ya saratani, homa ya ini, kifua kikuu, virusi vya Ukimwi (VVU) na vinasaba.

“Maabara inavyo vifaa vyote vya kisasa pamoja na watalaam na kwamba kwa mikoa  ya Kanda ya Ziwa uchunguzi wa magonjwa mengi utafanyika hospitalini hapa,” amesema Dk Massaga.

kusogezwa karibu kwa huduma za kupima Uviko-19 katika Hospitali ya Kanda ya Buganda kutasaidia kuokoa muda ambao watu walikuwa wanasubiri kupata majibu na hivyo kuutumia katika shughuli nyingine za biashara na safari za kimataifa ambazo zinatahitaji cheti cha ugonjwa huo.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Usimamizi na Maendeleo ya Afya (MDH),  Dk  David  Sando amesema kupitia ufadhili wa Marekani wameboresha maabara ya hospitali hiyo ambayo kwa sasa inaweza kupima Uviko-19  na kupata majibu kwa saa 24.

Amesema kabla ya kuboresha maabara hiyo, watu waliopimwa Uviko-19   kwa Kanda ya Ziwa sampuli zao zilitumwa Dar es  Salaam  na kulazimika kusubiri majibu kwa siku 3,  lakini kwa sasa kila kitu kitafanyika hapo.

Dk Sando amesema vifaa vilivyowekwa vimeongeza uwezo wa upimaji wa kila mwaka hadi zaidi ya vipimo milioini 1.17  vya pamoja vya VVU.

“Tunafuraha kuripoti kwamba katika kipindi cha miezi 12 iliyopita maabara hiyo imepima zaidi ya wateja 273, 000 kwa wingi wa virusi vya Ukimwi bila mrundiko wa sampuli,” amesema Dk Sando.

                         

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), hadi kufikia Novemba 8, 2021 Tanzania imeripoti wagonjwa 26,196  wa Uviko-19 na vifo 725.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel amesema kinachofanywa na Serikali ya Marekani ni masuala ya kimapinduzi katika sekta ya afya yanayosaidia kurahisisha matibabu kwa Watanzania.

“Haya  mambo ni ya kimapinduzi unamfundisha mtu na unampatia nyenzo ya kuinuka moja kwa moja, hivyo kuna haja ya  kuushukuru ubalozi huo kwa mashirikiano ya kipekee kati ya Taifa letu na Marekani,” amesema Mhandisi Gabriel.

Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Dk Donald  Wright amesema  lengo la mahusiano hayo ni kuhakikisha wananchi wa Tanzania na mikoa ya Kanda ya Ziwa wanaendelea kunufaika na kuwa na afya njema.

”Serikali ya Marekani imekuwa ikisaidia Serikali ya  Tanzania kwa miaka mingi na imedhamilia kuboresha afya za Watanzania  pamoja na  kuimarisha mahusiano, kupambana na malaria, kifua kikuu,  VVU,  uzazi wa mpango,  Ebora  na magonjwa mengine,” amesema Balozi Wright.

Makala hii imefadhiliwa na Shirika la maendeleo ya habari la International Media Support (IMS) na Umoja wa Ulaya (EU).

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW