Bei za vyakula hazishikiki sokoni jijini Mwanza
- Zimepanda kwa viwango tofauti.
- bei za viungo yashuka.
- Sababu kuu ni kushuka kwa uzalishaji kulikosababishwa na ukosefu wa mvua.
Mwanza. Bei za bidhaa za vyakula katika masoko ya jijini Mwanza zimeendelea kupanda huku sababu kupungua kwa uzalishaji wa mazao kulikotokana na upungufu wa mvua katika msimu huu wa kilimo.
Sababu nyingine ni Serikali kufungua mipaka ambapo vyakula vingi kama mchele, mahindi na maharage vimekuwa vikiuzwa nje ya nchi.
Nukta Habari (www.nukta.co.tz) imezungumza na baadhi ya wafanyabiashara katika soko la Mchafukuoga jijini hapa ambapo wamesema kwa sasa bidhaa za vyakula zimepanda na kuiomba Serikali kuangalia namna ya kuwasaidia wananchi kudhibiti mfumuko huo wa bei.
Janeth Mussa, mfanyabiashara katika soko hilo amesema kwa sasa kilo moja ya mahindi yaliyokobolewa inauzwa Sh1,300 kutoka Sh800 miezi mitatu iliyopita huku kilo moja ya mchele supa ikiuzwa Sh2,200 kutoka Sh18,00 katika kipindi hicho.
“Kwa sasa hatupati faida, wateja wanalalamika kwa kuwa wamezoa bei ya zamani sahani moja ya wali mseto wa maharage ni Sh1,000 wakati kwa sasa tunawauzia Sh1,500,” amesema mama lishe huyo.
Bei ya sahani moja ya makande iliuzwa kuanzia Sh500 lakini kwa sasa inauzwa Sh1, 000 katika migahawa mingi kutokana na kupanda kwa bei za vyakula.
Janeth anasema bidhaa za vyakula havishikiki na kwamba hali ikiendelea hivi vitapanda zaidi.
Mussa Masanja ni mfanyabiashara wa mahindi katika soko la wakulima la Buhongwa amesema kwa sasa debe moja la mahindi linauzwa Sh15,000 kutoka Sh10,000 huku gunia moja likiuzwa Sh90,000 kutoka Sh60,000 ya zamani.
“Bei hii ya mahindi inatofautiana kulingana na umbali mfano walioko wilayani kama Kwimba na Magu wao wananunua mahindi kwa bei ya juu zaidi ya hapa utakuta debe moja linauzwa Sh20,000 na gunia moja likiuzwa Sh120,000,” amesema Masanja.
Soma zaidi:
-
Soko la Soni: Kivutio kingine cha utalii wilayani Lushoto
- Wafanyabiashara, wakulima waneemeka bei ya maharage ikipanda
Mwenyekiti wa Soko Kuu la Mwanza, Ahmed Nchora amekiri kuwa bei za bidhaa zimepanda lakini bei za viungo vya mboga zimeshuka.
Nchora amesema sababu kubwa ya bidhaa kupanda ni msimu wa kilimo kutokuwa mzuri kutokana na mvua kuwa chache hivyo uzalishaji kuwa mdogo.
Amesema wakulima wengi hutegemea mvua na hawalimi kilimo cha umwagiliaji, hivyo uzalishaji kuwa hafifu.
Nchora amesema kilo moja ya mchele supa ni Sh2,200 huku wa kawaida ni Sh1,800.
Bei hizi zimedumu kwa muda wa miezi mitatu sasa toka mwezi wa tatu,
Katika soko hilo, Nchora amesema maharage yanauzwa Sh2,000 kwa kilo. Unga wa mahindi ni Sh1,300 kwa kilo moja kutoka Sh800.
Bei ya viazi mviringo nayo imepanda kutoka Sh800 kwa kilo hadi Sh1,000 na kwamba viazi hivi kwa sasa vinatoka nchini Kenya badala ya Mbeya na Tarime mkoani Mara.
Mwenyekiti huyo amesema mbali na vitu hivyo kupanda baadhi ya bidhaa kama mboga mboga na viungo vimeshuka bei, akitolea mfano gunia moja la vitunguu la kilo 150 kwa sasa linauzwa Sh100,000 kutoka Sh350,000 miezi mitatu iliyopita.
“Hali kadhalika nyanya, hoho na viungo vingine vya mboga vimeendelea kushuka bei, changamoto ni bei za vyakula kila kukicha bei inapanda,” amesema Nchora.
Tangazo:

Latest