Bei ya wanyamapori yagonganisha vichwa mawaziri Afrika
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro akizungumza na jambo na Waziri wa Utalii wa Gambia, Hamat Bah mara baada ya Mkutano wa Kimataifa wa 64 wa Utalii Kanda ya Afrika ulioandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii (UNWTO) unaoendelea kufanyika katika kisiwa cha SAL nchini Cape Verde.
- Ni kutokuwa na bei zinazolingana za wanyama hao.
- Imesababishwa nchi za Afrika kukosa mapato.
- Afrika yajipanga kutoa msimamo wa pamoja.
Dar es Salaam. Waziri wa Maliasili na Utalii Dk Damas Ndumbaro amezitaka nchi za Afrika kuwa na kauli moja kuhusu taratibu na bei za wanyamapori katika biashara ya uwindaji wa kitalii.
Dk Ndumabara ametoa wito huo alipokuwa akizungumza kwa nyakati tofauti katika vikao vya ana kwa ana na baadhi ya mawaziri wa utalii wa nchi za Afrika katika mkutano wa 64 wa kimataifa wa utalii uliondaliwa na Shirika la Umoja wa Kimataifa la Utalii Duniani (UNWTO) unaofanyika kwa muda wa siku nne nchini Cape Verde.
“Utofauti wetu huu umekuwa ukitukandamiza kama nchi kwani tulitakiwa sisi ndio tupange bei lakini kutokana na kutokuwa na umoja bei za wanyama zimekuwa zikiamuliwa na wao hili lazima tulikatae kwa kuungana kwa pamoja,” amesema Dk Ndumbaro.
Amezitaka nchi zote zinazoendesha utalii wa uwindaji zifanye mkutano kwa njia ya mtandao ili kujadili mustakabali wa biashara hiyo na kisha zitoke na kauli moja ili kuwathibiti wawindaji wa kitalii kwa ajili ya maslahi mapana ya uhifadhi barani Afrika.
Nchi zinazofanya vizuri katika uwindaji wa kitalii ni pamoja na Botswana, Zimbabwe, Tanzania, Zambia na Afrika Kusini
Kauli hiyo imeungwa mkono na Waziri wa Utalii wa Zimbabwe, Ngoghithize Ndlovu na amezitaka nchi hizo kuwa kitu kimoja katika kuamua kupanga bei za uwindaji wa kitalii.
Amesema bei za wanyama wanaoruhusiwa kuwindwa pamoja na vitalu vya uwindaji wa wanyamapori zimekuwa zikitofautiana sana kati ya nchi na hali hiyo imekuwa kikwazo kikubwa kwa shughuli uhifadhi barani Afrika.
Kutokana na kutofautiana kwa bei na baadhi ya kanuni na taratibu hizo, wawindaji wa kitalii wamekuwa wakitumia mwanya huo kuzikandamiza nchi za Afrika kwa kupanga bei wanazotaka wao huku wakidai kuwa bei hizo cha chini zimekuwa katika nchi nyingine pia.
Katika hatua nyingine, Dk Ndumbaro ametoa ahadi kwa Zimbabwe kama itakuwa tayari ipewe mafunzo ya kuendesha biashara ya uwindaji wa kitalii kwa mfumo wa digitali ambao utasaidia kuongeza mapato katika nchi hiyo.
Amesema tangu kuanzishwa kwa mfumo huo nchini Tanzania umeleta manufaa makubwa kwa nchi ambapo wawindaji wa kitalii ili kuweza kupata vitalu vya uwindaji wamekuwa wakilazika kushiriki katika mnada wa kimtandao.