Ahueni: Serikali yaeleza mikakati soko la mahindi ya Tanzania

May 3, 2021 7:37 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Yasema inafanya mazungumzo na Kenya ili kuruhusu mahindi kuuzwa nchini humo.
  • Inatoa vibali bure kwa wafanyabiashara wanaotaka kuuza mahindi nje ya nchi.
  • Inakusudia kuiongezea uwezo Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) inunue mazao mengi ya wakulima.

Dar es Salaam. Huenda wakulima nchini Tanzania wakapata ahueni kwa mahindi yao kupata soko siku za hivi karibuni baada ya Serikali kutangaza mikakati inayochukua kuwatafutia soko la uhakika ndani na nje ya nchi. 

Hatua hiyo imekuja baada ya kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa wakulima ya kuwa na mahindi mengi yaliyokosa soko na hivyo kuwaweka katika hatari ya kupata hasara. 

Malalamiko hayo, pia yameibuliwa bungeni leo Mei 3, 2021 na Mbunge wa Viti Maalum, Pindi Chana ambaye ameiomba Hifadhi ya Taifa ya Chakula (NFRA) kwenda kununua mahindi ili kuwaondolea wakulima adha wanayoipata sasa. 

Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe akitolea ufafanuzi wa suala hilo amesema kwa sasa NFRA haina uwezo wa kununua mahindi ya wakulima lakini ipo mikakati inayofanyika kufungua soko la zao hilo nje ya nchi. 

“Hatua za awali ambazo tumefanya, baada ya muda mfupi tutalitatua tatizo la biashara kati ya sisi na nchi ambayo imekuwa ikinunua mahindi kwa muda mrefu ya Kenya. Naamini soko hilo likifunguka litaongeza idadi mahindi yanayokwenda nje,” amesema Bashe. 

Bashe ambaye pia ni Mbunge wa Nzega Mjini, amesema wanafanya  mazungumzo na Mpango wa Chakula Duniani (WFP ambao wameonyesha nia ya kununua mahindi zaidi ya tani 150,000 za mahindi. 


Zinahusiana: 


Aidha, Bashe amesema kwa sasa wanatoa vibali bure kwa wafanyabiashara waliopata masoko nje ya nchi kwenda kuuza mahindi ya Tanzania. 

“Nitumie nafasi hii kuziomba halmashauri zisizuie mahindi, mpunga, mchele unaouzwa popote nje ya mipaka yetu kwa sababu kufanya hivyo itakuwa kutokumtendea haki mkulima,” amesisitiza Bashe wakati akijibu swali la Chana. 

Naibu Waziri huyo amesema wanafanya majadiliano na Wizara ya Fedha na Mipango ili  kuruhusu NFRA na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) kupata vibali vya kuchukulia fedha katika taasisi za fedha na kununua mazao mengi ya wakulima. 

“Niwaombe Watanzania watupe muda tunafanyia kazi hili jambo kuwajengea uwezo NFRA na CPB,” amesema Bashe. 

Huenda mikakati hiyo ya Serikali ikafufua matumaini ya Watanzania kuanza kufaidika na zao hilo la mahindi ambalo ni miongoni mwa mazao makuu ya chakula Tanzania. 

Ripoti ya Mapitio ya Uchumi kwa mwezi Machi 2021 (Monthly Economic Review) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inaeleza kuwa wastani wa bei ya jumla ya gunia la kilo 100 la mahindi mwaka ulioishia Februari 2021 ilikuwa ShSh51,450 ikiwa imeshuka kutoka Sh85,038 iliyorekodiwa Februari 2020.

Pia bei ya zao hilo la chakula imekuwa ikishuka mfululizo kwa miezi mitatu iliyopita tangu mwezi Novemba mwaka jana.  

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW