Ahueni, maumivu: Bei ya mchele ikipanda Dodoma
- Bei ya jumla ya zao hilo imepanda kwa Sh55,000 ndani ya kipindi cha wiki moja.
- Itakuwa kicheko kwa wafanyabiashara na maumivu kwa wanunuzi.
Dar es Salaam. Wafanyabiashara wa mchele katika jiji la Dodoma leo watalala na tabasamu baada ya bei ya jumla ya zao hilo kupanda kwa Sh55,000 ndani ya kipindi cha wiki moja.
Takwimu za mazao makuu ya chakula zilizotolewa leo (September 7, 2020) na Wizara ya Viwanda na Biashara zinaonyesha kuwa bei ya juu ya gunia la kilo 100 la zao hilo linauzwa kwa Sh220,000 katika soko la Majengo jijini humo ikiwa imepanda kutoka Sh165,000 iliyorekodiwa Jumatatu Agosti 31, 2020.
Hiyo ni sawa na kusema wafanyabiashara hao wataweka kibindoni Sh55,000 kwa kila gunia moja la mchele wanalouza leo sokoni.
Pia takwimu hizo ambazo hutolewa mara tatu kwa wiki, zinaonyesha kuwa bei ya chini ya mchele jijini humo imepanda hadi Sh160,000 kutoka Sh110,000 iliyorekodiwa wiki iliyopita katika soko hilo hilo la Majengo.
Kwa bei hizo zinazotumika leo, itakuwa ni maumivu kwa wanunuzi na kicheko kwa wafanyabiashara ambao kupanda kwa bei za mazao ndiyo faida kwao.

Latest