Pasipoti ya Tanzania yaingia 12 bora Afrika kwa uwezo wa kusafiri
- Pia imeshika nafasi ya 39 katika kipimo cha ukarimu kati ya nchi 199.
Dar es Salaam. Tanzania imeendelea kuimarisha nafasi yake katika ramani ya usafiri wa kimataifa, baada ya pasipoti yake kutajwa kuwa miongoni mwa pasipoti zenye nguvu zaidi barani Afrika na duniani.
Kwa mujibu wa ripoti ya ‘Passport Reports’ Tanzania imeshika nafasi ya 12 barani Afrika na nafasi ya 121 duniani ikizipiku nchi nyingine maarufu duniani.
“Pasipoti ya Tanzania inashika nafasi ya 121 duniani. Raia wa Tanzania wanaweza kusafiri katika nchi 43 bila kuhitaji visa, huku nchi 26 zikitoa visa wanapowasili,” imesema sehemu ya taarifa ya ripoti hiyo.
Hata hivyo, ripoti hiyo imebainisha kuwa bado Mtanzania mwenye pasipoti atahitaji visa kusafiri katika mataifa 125 ikiwamo Marekani, China, Canada, Australia, Ufaransa na Japani.
Kiwangio hicho cha uhitaji wa visa kwa Mtanzania mwenye pasipoti anaposafiri kimeongezeka kutoka nchi 111 zilizorekodiwa mwaka 2025.

Nguvu ya pasipoti hupimwaje?
Passport reports hupanga pasipoti kwa kutumia alama ya uwezo wa kusafiri (Mobility Score).
Alama hiyo inaonyesha jumla ya idadi ya nchi ambazo mtu anaweza kuingia bila visa, kwa kupata visa anapowasili (Visa on Arrival), au kwa kutumia kibali cha kielektroniki cha kusafiria (Electronic Travel Authorization – eTA).
Kulingana na ripoti hiyo, Tanzania imezipiku baadhi ya nchi za Afrika Mashariki kama Rwanda iliyoshika nafasi ya 17, Uganda (18), Burundi (46), Sudani Kusini (52) na Somalia (54) na Jamhuri ya Kidemokrasia Congo (DRC) iliyoshika nafasi ya 47.
Mbali na kupima uwezo wa Watanzania kusafiri nje ya nchi, ripoti pia imeangalia urahisi wa wageni kuingia Tanzania.
Katika kipimo hicho cha ukarimu, Tanzania imewekwa katika nafasi ya 39 kati ya nchi 199. Kipimo hicho kinahusu urahisi wa kuingia Tanzania kwa wenye pasipoti za kigeni na ni tofauti na kipimo cha nguvu ya pasipoti ya Tanzania.

‘Caribbean inaongoza kwa ufikiaji’
Licha ya Afrika kuwa miongoni mwa maeneo yenye ufikiaji mkubwa, Karibiani ndiyo inayoongoza katika ufikiaji wa pasipoti ya Tanzania kwa asilimia 81.3.
Ripoti inaonyesha kuwa Karibian ina nchi 11 zisizohitaji visa, nchi moja katika kundi la visa ya kuwasili au taratibu zilizorahisishwa, nchi moja yenye idhini ya kielektroniki ya kusafiri na nchi tatu zinazohitaji visa.
Amerika Kaskazini inafuata kwa asilimia 52.2, Oceania asilimia 50, Asia asilimia 30 na Amerika Kusini asilimia 25, Mashariki ya Kati asilimia 5.9, wakati Ulaya, nchi za Ghuba na Asia ya Kati ina asilimia sifuri mtawalia.