‘Norovirus’: Virusi vinavyoua maelfu ya watoto kila mwaka
- Vifo 50,000 sawa na robo ya vifo vyote vinahusisha watoto pekee kila mwaka.
- Husababisha takribani visa milioni 685 vya maambukizi kila mwaka duniani kote.
Dar es Salaam. Kuharisha na kutapika ni miongoni mwa magonjwa yanayoripotiwa mara kwa mara hususani kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano.
Baadhi ya wazazi huihusisha hali hiyo na maendeleo ya ukuaji wa mtoto ikiwemo kuota meno, kutambaa au kutembea, bila kujua kuwa inaweza kuwa dalili ya maambukizi ya virusi ikiwemo ‘Norovirus’.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) ‘Norovirus’ ni virusi vinavyoshambulia tumbo na utumbo, hali inayojulikana kitaalamu kama ‘acute gastroenteritis’.
Kinachofanya ‘Norovirus’ kuwa hatari si tu dalili zake, bali uwezo wake wa kuenea kwa urahisi kupitia chakula, maji au hata kugusa sehemu zilizochafuliwa na virusi hivyo.
WHO inasema virusi hivyo husababisha takribani visa milioni 685 vya maambukizi kila mwaka, huku karibu asilimia 29 ya wagonjwa wakiwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano.
Ugonjwa huo pia, husababisha takribani vifo 200,000 ambapo vifo 50,000 sawa na robo ya vifo vyote vinahusisha watoto pekee kila mwaka.
Ugonjwa mgeni Tanzania
Dk Rashid Issa kutoka mkoani Tanga anasema hadi sasa ‘Norovirus’ ni ugonjwa unaoonekana mara chache nchini Tanzania ukilinganishwa na baadhi ya mataifa ikiwemo Marekani, ambako takribani visa milioni 21 huripotiwa kila mwaka.
Hata hivyo, wataalamu wa afya wanaonya kuwa uwezo wake wa kuenea kwa haraka unafanya kuwa muhimu kwa wananchi kufahamu hasa wakati ambapo milipuko ya magonjwa ya mfumo wa chakula unaendelea kuripotiwa katika mataifa mbalimbali duniani
“Norovirus si ugonjwa unaoonekana mara kwa mara nchini Tanzania. Unapotokea, mara nyingi huwa katika mfumo wa mlipuko, lakini bado ni nadra ukilinganisha na magonjwa mengine ya tumbo,” anasema Dk. Issa.
Dalili za ‘Norovirus
Dk Issa anabainisha kuwa dalili za Norovirus huanza ghafla, ambapo mgonjwa anaweza kuanza kutapika kwa nguvu na kuharisha mara kwa mara bila dalili za awali.
Anasema wagonjwa wengi pia hupata maumivu ya tumbo, kichefuchefu na wakati mwingine homa ya kiwango cha chini. Tofauti na baadhi ya maambukizi ya tumbo yanayosababishwa na bakteria, ‘Norovirus’ kwa kawaida husababisha kuharisha kusikoambatana na damu.
Hatari kubwa ya ugonjwa huo, Dk Issa anasema ni kupoteza maji mwilini kutokana na kutapika na kuharisha mfululizo jambo linaloweza kufanya midomo kukauka, macho kuzama ndani, ngozi kukosa unyevunyevu, kiu kali na kupungua kwa mkojo.
Anasisitiza kuwa watoto wadogo ndio wako kwenye hatari zaidi ya kupata madhara makubwa, hivyo wazazi na walezi wanapaswa kuwahi kuwapeleka hospitalini mara tu wanapoanza kuonyesha dalili hizi ili wapate matibabu mapema.
Kinga inaanzia kwenye usafi
‘Norovirus’ ni miongoni mwa virusi vinavyowezwa kuambukizwa kwa kula chakula au kunywa maji yaliyochafuliwa, kugusana na mtu aliyeambukizwa, kushika sehemu zenye virusi na kisha kugusa mdomo bila kunawa mikono na kuchangia vyombo vya chakula na mgonjwa.
Kwa kuwa hadi sasa hakuna dawa maalumu ya kutibu ‘Norovirus’, wataalamu wa afya wanasema kinga ndiyo njia bora ya kujilinda dhidi ya maambukizi.
Wanasisitiza kuzingatia usafi wa mazingira, kunawa mikono kwa sabuni na maji tiririka mara kwa mara, pamoja na kuhakikisha chakula kinaandaliwa na kuhifadhiwa katika mazingira salama.
Pia Dk Issa anashauri matunda na mboga zisafishwe vizuri kabla ya kuliwa, huku vyakula vya baharini kama chaza vikipikwa vizuri ili kuua vimelea vinavyoweza kusababisha maambukizi.
Mbali na usafi wa chakula, Dk Issa amewataka watu wanaopata dalili za kuharisha na kutapika kuwahi katika vituo vya afya kwa uchunguzi na matibabu ya mapema, badala ya kujitibu nyumbani.