Pato la Taifa kukua kwa wastani wa 6.3% mwaka 2026/27 Tanzania
- Wizara ya fedha yaomba Sh21.1 trilioni ili kufikia azma hiyo na kutimiza vipaumbele 8 bajeti 2026/2027.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema inatarajia kukuza pato la Taifa (GDP) kwa wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2026/ 27 kutoka wastani wa asilimia 5.9 uliopo sasa.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar aliyekuwa akiwasilisha hotuba ya mapendekezo ya bajeti ya wizara yake kwa mara ya kwanza bungeni tangu kuteuliwa kwake amesema ukuaji huo ni sehemu ya vipaumbele nane vya wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
“Kwa mwaka 2026/27, Wizara ya Fedha inatarajia kutekeleza vipaumbele vinane ambavyo ni pamoja na kusimamia kwa weledi uchumi jumla ili kufikia ukuaji wa asilimia 6.3 mwaka 2026” amesema Balozi Omar.
Ikiwa GDP ya Tanzania ambayo kwa sasa thamani yake inakadiriwa kuwa takriban Dola za Marekani 94.9 bilioni (takriban Sh250 trilioni) kwa mujibu wa IMF na Benki ya Dunia itakuwa kwa wastani unaotarajiwa, itakuwa ni kwa mara ya tatu mfululizo kwa pato hilo kuongezeka kwa wastani wa asilimia 0.4 kila mwaka.
Mwaka 2025, GDP ya Tanzania ilikuwa kwa asilimia 0.4 na kufikia wastani wa asilimia 5.9 kutoka wastani wa asilimia 5.5 mwaka uliotangulia.
Hata hivyo, wakati Serikali ikitarajia ukuaji wa asilimia 6.3 matazamio yapo tofauti kwa Benki ya Dunia ambayo inatarajia pato la Taifa la Tanzania kukua kwa wastani wa asilimia 6.2, asilimia 0.1 nyuma ya matarajio ya Serikali.
Licha ya matarajio hayo, yaliyoorodheshwa kwenye Ripoti ya Matarajio ya Uchumi wa Dunia 2026, Benki ya Dunia inaitaja Tanzania miongoni mwa nchi tatu bora za Afrika Mashariki ambazo uchumi wake unakua kwa kasi ikitanguliwa na Rwanda ambayo uchumi wake unatazamiwa kukua kwa asilimia 7.2 mwaka 2026.
Ili kufikia azma hiyo, Waziri Omar ameliomba bunge kuidhinisha bajeti ya Sh21.2 trilioni ili kutimiza vipaumbele vingine saba kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Vipaumbele hivyo vingine ni pamoja na kudhibiti mfumuko wa bei kubaki ndani ya tarakimu moja, kuimarisha nidhamu ya usimamizi wa fedha serikalini, kuboresha mifumo ya usimamizi wa mapato, misaada na mikopo, kulipa kwa wakati riba na mtaji wa deni la Serikali.