Dola yaimarika kwa Sh5 CRDB, Sh8 NMB, Mei 21, 2026
- Ni kwa siku ya tatu mfululizo sarafu hiyo inazidi kuimarika katika benki hizi mbili za kibiashara nchini.
Dar es Salaam. Dola ya Marekani yaendelea kuimarika dhidi ya Shilingi ya Tanzania kwa siku ya tatu mfululizo ikiongezeka kwa Sh5 katika benki ya CRDB na Sh8 NMB kwa bei ya kuuza na kununua.
Kwa mujibu wa takwimu za viwango vya kubadilisha fedha vya leo Mei 21, 2026, Dola ya Marekani katika benki ya CRDB inauzwa kwa Sh2,660 na kununuliwa kwa Sh2,580.
Hii ni sawa na ongezeko la asilimia 0.19 kulinganisha na Sh2,655 kwa bei ya kuuza na Sh2,575 kwa bei ya kununua zilizotumika hapo jana.
Hali kama hiyo imeonekana NMB ambapo leo Dola ya Marekani imeongezeka kwa Sh8 hadi kuuzwa kwa Sh2,663 kutoka Sh2,655 ya jana huku bei ya kununua ikipanda hadi Sh2,583 kutoka Sh2,575.
Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 0.3 kwa bei ya kuuza na kununua katika benki ya NMB ukilinganisha na viwango vilivyotumika jana Mei 20, 2026.

Hii inaonyesha kuwa wafanyabiashara na waagizaji bidhaa watakaotumia dola kupitia benki ya NMB watalazimika kutumia kiasi kikubwa zaidi cha fedha kulinganisha na jana, huku gharama zikiendelea kuwa nafuu kidogo kwa wanaobadilisha fedha kupitia CRDB.
Katika sarafu nyingine, Euro imeonyesha kushuka kidogo katika benki ya CRDB ambapo bei ya kununua imeshuka kutoka Sh2,883.8 hadi Sh2,877.51 na kuuza kushuka kutoka Sh3,183.8 hadi Sh3,177.51.
Kwa upande wa Sterling ya Uingereza, Shilingi ya Tanzania imeendelea kuimarika kidogo katika CRDB huku pauni ikiuzwa kwa Sh3,648.87 kutoka Sh3,652.2 ya jana.
Aidha, sarafu za kikanda ikiwemo Shilingi ya Kenya, Rand ya Afrika Kusini na Yuan ya China zimeendelea kubaki katika mabadiliko madogo, hali inayoashiria utulivu wa soko la fedha za kigeni nchini.