Rais Kagame kufanya ziara ya kikazi Tanzania kesho
- Ziara hiyo inalenga kuimalisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.
Dar es Salaam.Rais wa Rwanda Paul Kagame, anatarajia kufanya ziarra ya siku moja nchini Tanzania Kesho, Mei 3, 2026 ambapo pamoja na mambo mengine atafanya mazungumzo na Rais Samia Suluhu Hassan.
Taarifa ya Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu Bakari Machumu iliyotolewa leo Mei 2, 2026 inaeleza kuwa viongozi hao watajadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Rwanda.
“Katika ziara hiyo, Rais Kagame atafanya mazungumzo na mwenyeji wake, Rais Tanzania Samia Suluhu Hassan. Mazungumzo yao yataangazia masuala ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Ziara hiyo inaelezwa kuwa sehemu ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kihistoria na kidiplomasia uliopo kati ya mataifa hayo mawili ya Afrika Mashariki, ambayo yameendelea kushirikiana katika sekta mbalimbali za maendeleo na usalama wa kikanda.
Hii sio mara ya Kwanza kwa Rais Kagame kufanya ziara nchini Tanzania katika awamu ya ya uongozi wa Rais Samia kwa shughuli za kikazi na mikutano ya kikanda.
Mathalani mwaka 2023, aliwasili nchini kwa ziara za siku mbili, mwaka 2025 Rais Kagame pia alihudhuria mkutano wa pamoja wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Dar es Salaam kujadili hali ya usalama mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Hata hivyo, ukiachana na awamu ya Rais Samia pia aliwahi kufanya ziara ya siku mbili katika awamu za viongozi wengine akiwemo Hayati John Pombe Magufuli 2016 na Mwaka 2019.
Aidha, Tanzania na Rwanda zimeendelea kushirikiana kwa karibu katika miradi ya kimkakati ikiwemo matumizi ya Bandari ya Dar es Salaam kwa usafirishaji wa mizigo kwenda Rwanda pamoja na miradi ya reli na usafiri wa anga inayolenga kukuza biashara ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki.

Latest