Wizara ya Afya yatahadharisha uwepo wa COVID-19, Dengue, mafua makali Tanzania

February 25, 2026 12:31 pm · Fatuma Hussein
Share
Tweet
Copy Link
  • Yawataka wananchi kuchukua tahadhari juu ya magonjwa hayo ya mlipuko.
  • Imesisitiza kuwa itaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa hayo na kutoa taarifa kwa umma kadri itakavyohitajika.

Dar es Salaam. Wizara ya Afya imetoa tahadhari kwa wananchi kuhusu kuongezeka kwa maambukizi ya magonjwa ya mlipuko yakiwemo UVIKO-19, homa ya dengue na mafua makali ikiwataka kuchukua hatua za kujikinga ili kudhibiti kusambaa kwa magonjwa hayo.

Taarifa ya Mganga Mkuu wa Serikali Dk Grace Magembe iliyotolewa leo Februari 25, 2026 imefafanua kuwa tahadhari hiyo imetolewa kufuatia ongezeko la visa maeneo mbalimbali nchini.

Takwimu za ufuatiliaji zinaonesha kuwa, kila mwaka katika kipindi cha mwezi Novemba hadi Aprili kunakuwa na ongezeko la ugonjwa wa mafua makali ya Influenza na UVIKO-19 hapa nchini na duniani,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Dk Magembe.

Magonjwa hayo ya mlipuko ni miongoni mwa yale yaliowahi kuripotiwa nchini yakisababisha mamilioni ya watu kupoteza maisha ikiwemo Uviko -19 uliowasumbua Watanzania kwa miaka miwili kabla ya kuanza kutolewa kwa chanjo mwezi Julai 28, mwaka 2021 zilizosababisha kupungua kwa visa vipya vya ugonjwa huo.

Homa ya mafua husambaa kwa urahisi kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine hivyo kusababisha ugonjwa wa mlipuko. Picha/Canva.

Mbali na chanjo, Wizara ya Afya imewataka wananchi kuzingatia kanuni za afya ikiwemo kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni au kutumia vitakasa mikono, kufunika mdomo na pua wakati wa kukohoa au kupiga chafya, na kuepuka misongamano isiyo ya lazima.

“Hali hii inatutaka kila mmoja wetu kuchukua tahadhari, kuwahi katika kituo cha kutolea huduma za afya kupata matibabu stahiki, vile vile kuepuka kujitibu au kutumia antibiotiki bila ushauri wa wataalam wa afya,” inaeleza sehemu ya taarifa.

Kwa upande wa homa ya Dengue, ambayo huenezwa na mbu aina ya Aedes, wizara imeeleza kuwa imeendelea kuripotiwa katika baadhi ya maeneo hususan wakati wa msimu wa mvua. 

Ili kukabiliana na homa hiyo taarifa  ya Dk Magembe imewahimiza wananchi kutokomeza mazalia ya mbu kwa kuweka mazingira katika hali ya usafi, matumizi ya vyandarua, na kuvaa nguo ndefu kuzuia mbu.

Virusi vya Uviko-19 ni kundi kubwa la virusi ambayvo kwa kawaida hupatikana miongoni mwa wanyama na vinaweza kusababisha ugonjwa kwa wanyama na binadamu. Picha/Canva.

Tahadhari ya kipindupindu kuendelea

Katika taarifa hiyo pia Wizara ya Afya imewataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa kipindupindu licha ya kutokuwepo kwa wagonjwa ndani ya mwezi mmoja uliopita.

Hatua zilizosisitizwa ni pamoja na kunywa maji safi na salama yaliyochemshwa au kutibiwa kwa dawa maalum, kunawa mikono kwa sabuni kabla ya kula na baada ya kutumia choo, pamoja na kuzingatia usafi wa mazingira na vyakula.

Ni asilimia 80 tu ya visa vya homa ya dengue ndio dalili. Asilimia 20 iliyobaki haonyeshi dalili au dalili za ugonjwa huo. Picha/Canva.

Wizara ya Afya imesisitiza kuwa itaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa hayo na kutoa taarifa kwa umma kadri itakavyohitajika, huku ikitoa wito kwa wananchi kushirikiana na mamlaka za afya katika kudhibiti na kuzuia milipuko.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks