Slivery Luboja Ambwaga Mnyeti Kura za Maoni Misungwi
- Apata kura 3,249 kati ya zaidi ya 15,000 zilizopigwa na wajumbe
Mwanza. Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Misungwi na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Alexander Mnyeti, amekiri kushindwa katika kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM) za kuwania nafasi ya ubunge wa jimbo hilo, akieleza kuwa sasa atajielekeza kwenye shughuli nyingine za kujipatia kipato.
Mnyeti, ambaye alichaguliwa mwaka 2020 baada ya kumshinda aliyekuwa mbunge wa wakati huo, Charles Kitwanga, alipata kura 3,249 kati ya kura zaidi ya 15,000 zilizopigwa na wajumbe wa jimbo hilo.
Katika uongozi wake, aliteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, nafasi anayoshikilia hadi sasa.
“Matokeo ndiyo hayo na mimi nimeyapokea kwa mikono miwili. Nilimshinda mtu na mimi nimeshindwa na mtu, na ndiyo utaratibu wa Chama Cha Mapinduzi; tunashindana kwa kura na mwenye kura nyingi ndiye mshindi. Nawashukuru wananchi kwa kunipa miaka mitano,” amesema Mnyeti.
Amesema kazi siyo ubunge pekee, kwani zipo fursa nyingi nyingine zikiwemo kilimo, uvuvi na biashara, ambazo atajihusisha nazo baada ya kumaliza kipindi chake cha ubunge.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Misungwi, Emmanuel Masangwa, mshindi wa kura za maoni ni Slivery Luboja aliyepata kura 9,684, akifuatiwa na Mnyeti (3,249).
Washindani wengine walikuwa John Kilangi (258), William Kafiti (202), Deusdediti Komanya (136) na Isa Lufungulo (85).
“Tunashukuru uchaguzi umekuwa huru na haki. Sasa jukumu limebaki kwa Kamati ya Maadili ya chama ambayo itatangaza mgombea halali atakayewakilisha CCM katika uchaguzi ujao,” amesema Masangwa.