Dk Biteko akemea wizi wa miundombinu ya umeme Tanzania

December 11, 2024 7:01 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • Asema uharibifu na uhujumu wa miundombinu ni chanzo cha watu wengi kukosa umeme.

Dar es Salaam: Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dk Doto Biteko amesema Serikali ya Tanzania haita mvumilia yeyote atakaye jihusisha na uharibifu wa miundombinu ya umeme na atakayebainika atachukuliwa hatua.

Dk Biteko ameyasema hayo katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 400 kutokea Chalinze hadi Dodoma iliyofanyika leo Disemba 11, 2024 mkoani Dodoma.

Akizungumza katika hafla hiyo Dk Biteko amesema “tusicheke na wezi na kwa kweli mheshimiwa waziri wa mambo ya ndani nimefurahi ulivyosema olewao wanaofanya hii kazi” amesema Biteko akionyesha kusikitishwa na tabia ya baadhi ya watu kuingiwa na tamaa na kisha kuiba miundombinu ya umeme kama vile nyaya za umeme na mafuta ya vipozeo vya umeme na kwenda kuviuza.

Kwa mujibu wa Dk Biteko kati ya mwezi  Julai 2023 mpaka Septemba mwaka huu jumla ya matukio 35 ya wizi wa miundombinu ya umeme yameripotiwa huku mengine 23 yakiripotiwa kati ya mwezi Oktoba na  Novemba mwaka huu.

Dk Biteko amefafanua kuwa uharibifu na uhujumu wa miundombinu hiyo umesababisha treni za mwendo kasi (SGR) kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi unaotakiwa.

Kauli ya Dk biteko inakuja wakati safari za SGR zikiripotiwa kukwama katika maeneo tofauti kati ya kipande cha Dar es Salaam hadi Dodoma kilichozinduliwa mwezi Agosti mwaka huu kwa sababu zilizoelezwa kuwa ni hujuma katika miundombinu ya umeme.

Mtendaji Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Masanja Kadogosa Novemba mwaka huu alisema tayari wameshawabaini wanaohujumu miundombinu hiyo na tayari watuhumiwa sita wameshashikiliwa na Jeshi la Polisi

Ili kulinda miundombinu hiyo Dk Biteko ametoa wito kwa Watanzania katika kuhakikisha kila mmoja anakuwa mlinzi wa mwenzie na kutoa taarifa pale inapohitajika.

Pia ametoa agizo la kushikiliwa kwa mtu mmoja kutoka Mkoa wa Pwani aliyekutwa na shehena za miundombinu ya umeme kama nyaya na mataluma ya reli na kusisistiza sheria kufuatwa juu yake ili kukomesha vitendo hivyo.

Aidha, Dk Biteko amewahakikishia Watanzania kuwa Serikali ya Tanzania ni aminifu na inaweka mkazo sana katika suala la nishati ili kuhakikisha maendeleo ya viwanda na matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW