Viongozi wa dini walaani matukio ya ukatili Mwanza, washauri kurudi kwenye misingi ya kiimani
- Ni baada ya kukithiri kwa matukio ya ukatili mkoani humo.
- Waeleza sababu na jinsi jamii inavyoweza kupunguza matukio hayo.
Mwanza. Kufuatia matukio ya ukatili yanayoendelea kuripotiwa mkoani Mwanza, viongozi wa dini wamelaani vitendo hivyo na kushauri wananchi wa mkoa huo kurudi kwenye misingi ya kwanza ya kiimani.
Wakizungumza na Nukta Habari, viongozi hao wamesema miongozo ya kidini sheria na kanuni za nchi haziruhusu mtu yeyote kujichukulia sheria mkononi na iwapo kutatokea kutoelewana baina ya pande mbili ni vyema wakaenda mahakani kutafuta suluhu.
“Tunalaani matukio ya kikatili yanayoendelea kufanyika jijini Mwanza, hakuna mtu aliye juu ya sheria na iwapo kuna kutoelewana baina ya pande mbili ni vyema wakafikishana mahakamani ili kupata haki kuliko kujichukulia sheria,” amesema Askofu wa kanisa la Waadventista Wasabato Kanda ya Nyanza kusini Beatus Mlozi.
Naye Mratibu wa Kamati ya amani Mkoa wa Mwanza, Shekh Twaha Bakari amesema tuhuma zozote za wizi na zingine zinapaswa kufikishwa kwenye vyombo vya dola ili kupata usuluhishi.
Rai hiyo ya viongozi wa dini imekuja wakati jiji hilo likiripoti matukio ya mara kwa mara ya ukatili wa kijinsia na mauaji yanayotishia usalama wa wakazi wa jiji hilo.
Mathalani katika kipindi cha wiki moja ilizopita mkoani Mwanza kumeripotiwa matukio matatu likiwemo la watoto sita wa familia moja kudaiwa kumshambilia mama yao mzazi wakimtuhumu kuwaroga wajukuu zake.
Tukio lingine ni la mkazi wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki ambaye alibakwa hadi kufa lingine ni lile lilotokea hivi karibuni ambapo muajiri anadaiwa kumchoma mfanyakazi wake wa ndani kwa kosa la kuiba fedha.
Soma zaidi:Serikali yatoa matibabu bure kwa binti aliyechomwa moto Mwanza
Sababu zatajwa
Wakizungumzia matukio hayo, viongozi wa dini wamesema chanzo ni jamii kusahahu msingi wa kwanza wa malezi na elimu ambao unatakiwa kufanywa na familia.
“Familia au mzazi ndio msingi wa kwanza katika suala la malezi pale wanapowafundisha watoto wao maadili mema ndio hujenga jamii iliyobora kwa baadae, lakini hivi sasa wote wamesahau na kugeukia shughuli zao wenyewe,” amesema Mchugaji Joseph Mpina wa Kanisa la Wasabato Nyanza Kusini.
Kwa upande wa ukatili unaofanyika kwa wanandoa Mchugaji Mpina amesema sababu ni kuingia kwenye ndoa bila kupewa elimu au mafunzo ya kutosha huku wengine wwakikimbilia hatua hiyo bila kufahamiana vizuri.
“Zamani kulikuwepo na zile mila za kuwafunda watoto namna ya kuzungumza mbele za watu, lakini namna watakavyoishi ndani ya ndoa lakini hivi sasa mambo yanaenda ndivyo sivyo kwa sababu wapenzi wanafahamiana kwa muda mfupi na wanachukua na wote hawana elimu yoyote ya ndoa,” amesema Mchungaji Mpina.
Kiongozi mwingine wa dini ya kiislamu kutoka msikiti wa Ijumaa Mwanza, Husein Issa amewataka wazazi kuwa walimu wa kwanza katika kuwafundisha watoto wao haswa wanapofikia umri wa kuingia kwenye mahusiano wawape elimu ya kutosha kuhusiana suala zima la ndoa.
“Pia viongozi tuna nafasi kubwa katika kuisaidia jamii hususani kwa wanandoa wapya hasa wanapokuja kwetu kutaka kuunganishwa wapate baraka za ndoa, kabla ya kufanya hivyo wapewe elimu ya namna ya kuishi kwenye ndoa,” amesema Sheikh Issa.