Mauzo ya kahawa yaipatia Tanzania Sh283.7 bilioni
- Ni mauzo ya tani 66,646 ya kahawa ya msimu wa 2018/2019.
- Kiasi kilichouzwa ni asilimia 102.8 ya makisio ya uzalishaji wa tani 65,000.
- Serikali yasema itaendelea kuimarisha mifumo ya masoko kuwapatia tija wakulima.
Dar es Salaam. Serikali imesema mauzo ya kahawa katika msimu wa mwaka 2018/2019 yamewezesha kuliingizia Taifa dola za Marekani milioni 123 sawa na takriban Sh283.7 bilioni.
Naibu Waziri wa Kilimo, Omary Mgumba aliyekuwa akizungumza leo (Novemba 12, 2019) Bungeni amesema hadi kufikia mwisho wa msimu wa 2018/2019 kiasi cha tani 66,646 cha kahawa kiliuzwa ikiwa ni asilimia 102.8 ya makisio ya uzalishaji wa tani 65,000.
“Kati ya tani hizo zilizouzwa, tani 41,971 zimeuzwa kupitia minada ya kahawa na 24,575 zimeuzwa katika soko la moja kwa moja,” amesema Mgumba.
Mauzo hayo yaliwezesha kuliingizia Taifa takriban Sh283.7 bilioni yakiwa yameshuka ikilinganishwa na msimu wa 2017/2018 ambapo mauzo yalikuwa Sh341 bilioni
Huenda mapato yatokanayo na uuzaji wa kahawa yakaendelea kupungua hata katika msimu wa mwaka 2019/2020, baada ya Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB) kusema uzalishaji wa zao hilo utashuka kutokana na mzunguko mdogo na kuchelewa kwa mvua katika mikoa ya kanda ya kaskazini ikiwemo Kilimanjaro na Arusha.
Katika taarifa ya Hali ya Sekta ya Kahawa Tanzania iliyotolewa na TCB mwezi April 2019 inaeleza kuwa matarajio ya uzalishaji wa kahawa katika msimu ujao wa 2019/2020 yatakuwa tani 50,000 ambapo ni sawa na upungufu wa asilimia 23.6 ukilinganishai na uzalishaji wa mwaka 2018/2019.
Soma zaidi:
- Uzalishaji kahawa kuimarika msimu 2019/2020
- Mnada wa kahawa kuwanufaisha wakulima?
- Uzalishaji wa kahawa kushuka msimu ujao
Aidha, Serikali imewahakikishia wakulima wa kahawa nchini kuwa mifumo ya mauzo ya moja kwa moja pamoja minada katika mikoa ya Kilimanjaro na Songwe, Ruvuma, Njombe, Kagera inayotumika msimu wa 2019/2020 itaendelea kutumika nchini.
“Kutumika kwa mifumo hiyo itasaidia kuongeza kipato cha wakulima na Taifa kwa ujumla,” amesema Mgumba wakati akijibu swali la Mbunge wa Kyerwa, Innocent Bilakwate aliyetaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kahawa inaongeza kipato cha Taifa.
Inayofanya Serikali kuboresha zao hilo
Naibu Waziri huyo amesema Serikali ina mikakati mbalimbali kuhakikisha zao la kahawa linapata soko la uhakika lenye tija kwa wakulima ikiwemo kutoa elimu kwa wakulima kuhusu pembejeo, na kuongeza uzalishaji kwa upanuzi wa mashamba ya zao hilo.
Pia kuzalisha miche bora ya kahawa yenye kuhimili ukame, magonjwa na wadudu ili kuongeza tija kwa wakulima na kuhamasisha kanuni bora za kilimo kupitia maafisa ugani.
“Serikali inaendelea kuboresha mifumo ya masoko ya zao la kahawa kwa kufanya utafiti wa mahitaji ya soko, kuimarisha vyama vya ushirika, kusimamia mikataba baina ya wanunuzi na wakulima na kuhamasisha uzalishaji wa uafanisi wenye tija ili kupunguza gharama za uzalishaji,” amesema Mgumba.
Latest