“Startups” zaanza kutumia fursa iliyoachwa na Jumia Tanzania
- Zaanza kufungua maduka ya mtandaoni kutoa huduma kama za Jumia.
- Zapania kuzifanyia kazi changamoto za muda na usambazaji wa bidhaa kwa wateja.
Dar es Salaam. Huenda ukawa mmoja ya wapenzi wa kutumia maduka ya mtandaoni kuagiza na kununua bidhaa mbalimbali unapokuwa umetingwa au ukiwa katika mapumziko nyumbani.
Huduma hizi ni msaada mkubwa pale mtu anapokosa muda wa kwenda dukani, sokoni au hata hotelini kupata huduma mbalimbali anazozihitaji kwa muda muafaka.
Licha ya baadhi ya kampuni zinazoratibu biashara ya bidhaa na huduma mtandaoni ikiwemo ya Jumia kuondoka Tanzania kutokana na sababu mbalimbali, imeibuka kampuni nyingine ambayo inatoa huduma kama za Jumia.
Huenda ulikuwa unawaza baada ya Jumia, nani ataingia sokoni kukupa kile unachotaka, basi tovuti ya kuagiza na kununua bidhaa mtandaoni ya Piki inaweza kuwa imebeba majibu yako.
Piki iliyoanzishwa takriban wiki mbili zilizopita na vijana wa Tanzania, inamwezesha mtu kuagiza bidhaa mbalimbali kama chakula, vifaa vya nyumbani, vifaa vya kielektroniki na vinywaji mtandaoni na kuletewa mahali popote kwa muda mfupi.
Utaweza kupata huduma zote hizo kwa kutumia simu janja, tableti, na kompyuta hasa katika majiji makubwa ya Dar es Salaam, Mwanza na Arusha baada ya kuainisha eneo ulipo na kukubaliana na bei ya bidhaa husika.
Piki imekuja na maboresho mbalimbali ikiwemo kuongezwa kwa huduma ya usambazaji wa vifaa vya nyumbani, vifaa vya kielektroniki na vinywaji ambavyo viko mbali na chakula tofauti na ilivyokuwa kwenye “Jumia Food”.
Piki pia imefanya maboresho ya muda utakaomchukua mteja au mtu aliyeagiza bidhaa kusubiri mzigo wake anapokuwa ameagiza. Badala ya mzigo kumfikia mlengwa baada ya siku tatu ilivyo kwa kampuni nyingine, mteja anapata mzigo wake baada ya nusu saa.
- Mambo yatakayosaidia kukuza “startups” za Tanzania mwaka 2020
- Startups za Tanzania zilizotamba mwaka 2018.
- “Startups” za Tanzania zapewa somo la uwazi, uwajibikaji kuvutia mitaji ya uwekezaji.
Kwa sasa, huduma hiyo inapatikana kwenye simu zenye mfumo wa Android na inategemea kujitanua kwenda kwenye mfumo wa iOS mwishoni mwa wiki hii.
Mmoja wa waanzilishi wa tovuti hiyo, Emmanuel Charles ameiambia www.nukta.co.tz kuwa wanakusudia kuhakikisha mtandao wao unakuwa na kasi hasa katika kuimarisha mifumo ya usambazaji bidhaa kwa wateja baada ya kuagiza.
“Kwenye Jumia ilikuwa inamchukua mteja siku tatu kupata bidhaa ya kielektroniki aliyoagiza, kwa sasa hivi mteja anapoagiza simu au kifaa chochote anakipata ndani ya nusu saa,” amesema Charles.
Ili kuhakikisha wanawafikia wateja wanaogiza bidhaa kwa muda mfupi, wanawatumia wasambazaji wao wa bidhaa ambao wako karibu na maeneo ambayo wanaishi wateja.
Hata hivyo, Piki itakuwa na kibarua kigumu kuhakikisha huduma zake zinakuwa endelevu ikizingatiwa kuwa bado kuna changamoto kwa Watanzania kuchangamkia fursa za mtandaoni.
Jumia ilifungasha virago vyake na kuondoka Tanzania Novemba 27, 2019 kwa madai kuwa inaangazia masoko sehemu nyingine duniani.
Baadhi ya wataalam na wachambuzi wa masuala ya biashara waliambia www.nukta.co.tz kuwa zipo sababu nyingi zinazosababisha kampuni zinazoendesha biashara ya mtandaoni sifanikiwe ikiwemo uelewa mdogo kuhusu masoko na elimu ya juu ya teknolojia ya mifumo ya kidijitali bado ni changamoto kwa Watanzania wengi.
Latest