Hapana: Kigogo wa Amazon hajawakataza Waafrika kutumia barakoa
- Amezushiwa kuwa amesema barakoa zenye rangi ya bluu zinazotengenezwa Ulaya zina sumu.
- Jeff hajatoa tamko lolote kwenye mitandao yake ya kijamii akisema waafrika waache matumizi ya barakoa
- Tunashauriwa kufuata maelekezo kutoka kwa wataalamu wa Afya.
Dar es Salaam. Siyo kila ujumbe unaopata kwenye mitandao ya kijamii ni wa kweli, huenda umeshakutana na ujumbe kwenye mtandao wa WhatsApp ukipotosha watu juu ya barakoa zenye rangi ya bluu zikiwa na sumu kuingizwa barani Afrika.
Ujumbe huo uliopo kwenye mfumo wa maandishi unasema mwanzilishi wa kampuni ya Amazon Jeff Bezos amesema bilionea Bill Gates amepanga njama ya kusafirisha barakoa zenye sumu ili kuangusha uchumi wa Afrika baada ya kushindwa kupitia chanjo ya Corona.

Sehemu ya ujumbe huo unaosambazwa unasema “Dear Africans, avoid wearing any blue masks which are made in America and in Europe because the masks contain Suicidal Toxins”.
Ujumbe huo unamaanisha kuwa “Wapendwa waafrika, epukeni kuvaa barakoa zozote za blue zinazotengenezwa Ulaya kwasababu zina sumu inayoua.”
Hata hivyo, habari hiyo haina ukweli wowote kwa sababu, mpaka sasa hakuna taarifa yoyote iliyotolewa na Jeff kwenye vyombo vya habari wala mitandao yake ya kijamii akiwataka watu Afrika kujiadhari na matumizi ya barakoa kama usemavyo ujumbe unaosambazwa.
Zinazohusiana:
Nukta Fakti imefanya utafiti wake na kubaini kuwa mpaka sasa hakuna taarifa yoyote iliyoripotiwa na mamlaka za afya likiwemo Shirika la Afya Duniani (WHO) kuhusu kuwepo kwa barakoo zenye sumu ambazo zina madhara kwa binadamu.
Badala yake watu wanashauriwa kuendelea kutumia barakoa, ikiwa ni njia mojawapo ya kujikinga na COVID-19 hasa katika mikusanyiko ya watu.
Hata hivyo, ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona bado tunashauriwa kufuata masharti yanayotolewa na wataalamu wa afya pamoja na mamlaka husika.
Latest