Majaliwa: Tumebadilisha utaratibu wa kumuaga Rais Magufuli
- Amesema sasa mwili wa Hayati Rais Magufuli utazungushwa uwanjani na mitaani badala ya kila mwananchi kupita mbele ya jeneza.
- Amesema wameamua kufanya hivyo kutokana na idadi kubwa ya watu wanaojitokeza kumuaga.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imelazimika kubadilisha utaratibu wa awali wa kumuaga Hayati Rais John Magufuli kwa kila mtu kupita mbele ya jeneza badala yake mwili wake utazungushwa uwanjani na mitaani.
Mabadiliko hayo yamefanyika baada ya kujitokeza kwa idadi kubwa ya watu katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam na muda wa kuaga kwa kila mwananchi kutokutosha.
Utaratibu huo mpya wa kuzungusha mwili ulianza kutumika jana Machi 21 jijini Dar es Salaam ambapo ulizungushwa mara tano na kupitishwa katika barabara mbalimbali jijini humo kabla ya kusafirishwa hadi jijini Dodoma.
Majaliwa aliyekuwa akizungumza leo Machi 22, 2021 wakati wa kuaga mwili wa Hayati Magufuli katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma amesema utaribu huo mpya utatumika katika maeneo yaliyobaki ambapo mwili wa marehemu utapita.
“Tunachofanya ni kuuzungusha mwili uwanjani na kuupitisha mitaani ili kila mtu apate fursa ya kuaga,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi:
- Siku ya mwisho Rais Magufuli kuzungumza hadharani
- Rais Magufuli afariki dunia kwa maradhi ya moyo Tanzania
Hayati Dk Magufuli aliagwa kwa siku mbili jijini Dar es Salaam na leo anaagwa jijini Dodoma na kisha mwili wake utapelekwa Zanzibar, Mwanza na hatimaye Chato mkoani Geita ambako huko ndiko atakakozikwa Machi 26 mwaka huu.
Kwa wakazi wa Dodoma wanaaga mwili wa Magufuli katika viwanja vya Dodoma ambapo shughuli hiyo inahudhuriwa wananchi na viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wakiwemo marais zaidi ya 10 wa mataifa mbalimbali.
Latest
