Kilimo cha nanasi kuanza kuwaneemesha wakulima Tanzania

April 27, 2021 6:39 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Serikali inakusudia kuanza kuzalisha mbegu bora za zao hilo.
  • Kuwawezesha wakulima kuzalisha mananasi yanakidhi viwango vya ubora wa viwanda na masoko ya kimataifa. 
  • Zao hilo na matunda mengine yapewa kipaumbele na Wizara ya Kilimo. 

Dar es Salaam. Huenda wakulima wa mazao ya matunda hasa mananasi wakaanza kufaidika na soko la mazao yao baada ya Serikali kuandaa mpango wa kuzalisha mbegu bora zitakazosaidia kuzalisha matunda yanayokidhi mahitaji ya wanunuzi wa ndani na nje ya nchi.

Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amesema wizara yake kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) wanafanya utafiti na kuzalisha mbegu bora za mananasi ili yakidhi viwango vya viwanda vya ndani na masoko ya kimataifa.

“Hatua tunayochukua sasa hivi kama wizara, tumewaagiza TARI ili kuweza kuzalisha mbegu ambazo zitakidhi viwango vya viwanda kukidhi ubora unaostahili kuweza kumsaidia mkulima,” amesema Bashe leo Aprili 27, 2021 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Msukuma. 

Msukuma katika swali lake alitaka kufahamu Serikali ina mikakati gani ya kuwasaidia wakulima ili kupata soko la uhakika la mananasi.


Soma zaidi:


Bashe ambaye ni Mbunge wa Nzega Mjini amesema mazao ya matunda yakiwemo mananasi awali hayawakuwepo katika mazao ya kimkakati lakini kwa sasa wizara yake imeweka kipaumbele katika sekta hiyo ili kuwanufaisha wakulima.

“Changamoto tuliyonayo katika sekta ndogo ya matunda ikiwemo nanasi na machungwa kwa muda mrefu kumekuwa hakuna uwekezaji wa kutosha tuliofanya kama nchi kwa sababu lilikuwa halionekani kama ni eneo la kimkakati.

“Sekta ya matunda na mbogamboga imepewa kipaumbele kikubwa na tumeagiza TARI Siriani kuwa ndiyo kituo halisi kwa ajili ya kufanya tafiti ili mazao ya mananasi na machungwa yaweze kukidhi mahitaji ya soko la ndani na la kimataifa,” amesema Bashe. 

Hapa Tanzania, nanasi hustawi katika mikoa ya Pwani, Tanga, Mtwara, Lindi, Geita na Mwanza ambapo hutumika kama chanzo cha vitamin A na B, kutengeneza mafuta na juisi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW