Kivuko chaanza kufanya kazi baada ya kusimama kwa miezi 16
Kivuko cha Mv Sengerema katika Ziwa Victoria kikiwa tayari kwa ajili ya safari. Picha| Temesa.
- Ni kivuko kinachotoa huduma Ziwa Victoria.
- Kitarahisisha shughuli za usafiri wa abiria na mizigo.
Mwanza. Baada ya kusimama kwa takribani miezi 16 hatimaye kivuko cha Mv Sengerema katika Ziwa Victoria kimeanza kufanya baada ya ukarabati wake kukamilika.
Kivuko hicho ambacho hufanya safari zake kati ya Kigongo (Mwanza) na Busisi mkoni Geita kimekarabatiwa kwa Sh2.5 bilioni na kampuni ya Songoro Marine ambapo kimewekewa injini mpya mbili ambazo zitasaidia kivuko hicho kwenda haraka.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa), Japhet Masele amesema pamoja na kuwa katika eneo hilo la kuvuka la Kigongo-Busisi kunajengwa daraja lakini vivuko hivyo ambavyo kwa sasa ni vitatu vitabaki kuendelea kuvusha watu na bidhaa ambazo haziwezi kupita juu ya daraja.
Vivuko vingine vilivyopo kwenye eneo hilo ni Mv Misungwi pamoja na Mv Mwanza.
Kwa mara ya kwanza kivuko hicho cha Mv Sengerema kiliundwa mwaka 1986 ambapo kina uwezo wa kubeba abiria 490, magari 20 na tani 70 za mizigo ambazo zinajumuisha magari na abiria.
“Ni kivuko cha nne kwa ukubwa kati ya vivuko vyote vinavyomilikiwa na Temesa na kuwa vivuko hicho na vingine vilivyopo vinachangia asilimia 15 ya pato la taifa,” amesema Masele wakati wa uzinduzi wa safari za kivuko hicho leo Agosti 19, 2021.
Kwa mujibu wa Masele mwaka 2018/19 vivuko vilichangia Sh1.2 bilioni.
Amewataka wananchi kuvitunza vivuko hivyo ili vitumike kwa muda mrefu.
“Songoro tumeshajenga vivuko vingi na serikali imeendelea kutuamini, hivyo tutaendelea kuonyesha uaminifu huo kwa kujenga vivuko kwa wakati,” amesema Tumbo Ndezero ni mwakilishi wa kampuni ya Songoro Marine.
Baadhi ya wasafiri waliozungumza na Nukta habari wamesema ujio wa kivuko hicho utapunguza msongamano na kupunguza muda wa kukaa kivukoni kusubiri.
“Zamani kulikuwa na vivuko viwili ambavyo vilikuwa vinachukua muda mrefu lakini kwa sasa vimefika vitatu ambavyo vitafanya kazi kwa urahisi zaidi,” amesema Anastazia Mashauri, mkazi wa jijini hapa.
Latest