Mapinduzi: Gari inayopaa angani kuanza safari mwaka 2023
- Ni gari aina ya “AirCar V5” limetengenezwa na kampuni ya Klein Vision ya nchini Slovakia.
- Lina uwezo wa kusafiri hadi maili 600.
- Lina beba abiria wawili na mzigo wa zaidi ya kilo 200.
Dar es Salaam. Jitihada za kuleta mapinduzi kwenye historia ya magari zimeanza tangu zamani. Tovuti ya How Stuff Work ya nchini Marekani inamtaja Glenn Curtiss kuwa “Baba wa magari yanayopaa” baada ya kubuni gari aina ya Curtiss Autoplane mwaka 1917.
Huenda ndoto za Curtiss zimepata wakuziendeleza kwani mitandao ya kijamii hivi karibuni ilizizima kwa kutangazwa kwa ujio wa gari linalopaa.
Gari hilo lililopewa jina la “AirCar V5” limetengenezwa na kampuni ya Klein Vision ya nchini Slovakia. Limefanyiwa majaribio tangu Juni 2021 ambapo liliweza kupaa kutoka uwanja wa ndege wa Nitra hadi uwanja wa ndege wa kimataifa wa Bratislave wa nchini Slovakia.
Kwa umbali huo AirCar V5 ilitumia dakika 35 kumaliza safari yake huku kwa safari ya gari la kawaida, umbali huo (kilomita 90) huchukua dakika 57 hadi saa moja.
Majaribio hayo yameipima gari hiyo uwezo wake wa kutua na kupaa kwa zaidi ya mara 200 na kukidhi vigezo vya Shirika la Usalama wa Anga la Ulaya (EASA).
“AirCar imetengenezwa kwa kutumia injini ya 1.6L kutoka kwenye kampuni ya kutengeneza magari ya BMW na inatumia mafuta yanayopatikana kwenye sheli yoyote ya kuuza mafuta,” amesema mwanzilishi mwenza wa Klein Vision, Anton Zajac.
Hata hivyo, mwenyekiti wa jamii ya wataalamu wa matengenezo ya vyombo vya usafiri vya angani, Kyriakos Kourousis amesema siyo mara ya kwanza vyombo vya usafiri vya aina hiyo vinapewa ithbati (kibali).
Sokoni hatua kwa hatua
Baada ya majaribio ya muda mrefu, kampuni ya Klein Vision, imetangaza kuwa AirCar imepewa kibali kama chombo cha angani (airworthy) baada kufanyiwa majaribio kwa muda mrefu.
Msemaji kutoka Klein Vision, ameliambia Shirika la Habari la CNN kuwa baada ya ithbati hiyo, gari hilo litakuwa sokoni ndani ya miezi 12, hivyo huenda Februari 2023 tukawa tunazungumzia mambo mengine.
Hata hivyo, siyo kila mtu ataweza kutumia gari hizo kwani zinahitaji mtu awe na leseni ya kuendesha gari hilo lenye kazi mbili yaani kutumika ardhini na angani pia.
Kinachokuja na AirCar
Gari hilo linaloambatana na uwezo wa kupaa hadi futi 18,000 lina uwezo wa kujibadilisha kutoka gari na kuwa ndege ndani ya dakika tatu.
AirCar ina uwezo wa kusafiri hadi maili 600 likiwa na nafasi za abiria wawili na uwezo wa kubeba mzigo wenye uzito wa kilogramu 204.1.
Uko tayari kupanda gari la angani?
Latest
