Jinsi Tanzania inavyoweza kuongeza upatikanaji wa haki za binadamu
- Ni pamoja na kutoa elimu ya haki za binadamu kwa wasiofikiwa.
- Serikali kuridhia mabadiliko ya sheria mbalimbali zinazokandamiza haki za binadamu.
Dar es Salaam. Wakati dunia ikiadhimisha miaka 75 ya tamko la ulimwengu la haki za binadamu, wadau na wanaharakati wametoa mapendekezo yatakayoimarisha upatikanaji wa haki hizo nchini.
Maadhimisho ya tamko la ulimwengu la haki za binadamu huadhimishwa kila Disemba 10 duniani kote ambapo kila nchi wanachama kukutana kusherehekea na kujadili ustawi wa haki hizo katika nchi zao.
Kwa mwaka huu, maadhimisho hayo yaliyoandaliwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) yamefayika leo Disemba 8, 2023 jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wadau, wanaharakati na watetezi wa haki za binadamu kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Baadhi ya wahudhuriaji wa maadhimisho ya miaka 75 ya tamko la haki za binadamu yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.Picha|Lhrc.
Mkurugenzi wa Shirika la haki za wasichana (Her initiative) Rebeca Gyumi, aliyekuwa miongoni mwa wanajopo katika mdahalo uliokuwa sehemu ya maadhimisho hayo, amesema ili kuhakikisha ustawi wa haki za binadamu nchini ni vyema wadau, wananchi na wanaharakati kuendeleza mapambano ili kuzipata.
“Hakuna haki zinazopatikana kirahisi…ni vyema tuendelee kuzipigania haki zetu na tuzilinde na tuzipozilinda tutarudi mwanzo,” amesema Gyumi.
Naye Helen Kijo Bisimba, Mwanaharakati na Mkurugenzi mstaafu wa Lhrc ametoa rai kwa mashirika yasiyo ya kiserikali kuongeza kasi ya utoaji wa elimu ya haki za binadamu kwa wananchi husasani maeneo yasiyofikiwa ili waweze kuzitetea.
“Tunatakiwa kuwasaidia watu wajue haki zao, tukiwasaidia wakizijua hakika watajitetea,” ameongeza Bisimba.
Maoni mengine ya jinsi ya kuhakikisha ustawi wa haki za binadamu nchini yalliwasilishwa na Mwenyekiti wa tume ya haki za binadamu na utawala bora Mathew Maimu, aliyetoa wito kwa Serikali kuridhia mabadiliko ya sheria mbalimbali zinnazokandamiza haki za binadamu.
Miongoni mwa sheria hizo ni pamoja na sheria ya ndoa ya mwaka 2009 inayoruhusu mtoto wa kike kuolewa akiwa umri wa miaka 14 kwa idhini ya wazazi jambo linalozuia upatikanaji wa haki kwa kundi hilo.
Soma zaidi:DCEA kutumia mbinu shirikishi kukabiliana na dawa za kulevya Tanzania
Jitihada zaidi zinahitajika
Aidha, Mkurugenzi wa Lhrc, Anna Henga aliyekuwa akizungumza katika maadhimisho hayo amesema licha ya hatua ambazo Tanzania imezipiga katika upatikanaji wa haki za binadamu bado jitihada zaidi zinahitajika ikwemo kutekeleza malengo endelevu yanayohusisha haki hizo.
“Yale malengo endelevu yatekelezwe sio katika maandishi tuu…kuna makundi ambayo haki zao zimeminywa kuliko mengine ikiwemo watoto, wanahabari, wanaharakati wa haki za binadamu,” amesema Henga.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo ikiwa wananchi na wanaharakati na wadau mbalimbali wa haki za binadamu wakishirikiana kwa pamoja wanaweza kutengeneza jamii yenye utoshelevu wa haki hizo.
“Tumejadiliana kwamba angalau tukifika miaka 100 ya haki za binadamu tuwe na usawa wa kijinsia, tuwe na amani na haki za binadamu Ifikie hatua ambapo kila mtu anafurahi, amesema Henga.
Latest