Guterres: Tuungane kuwasaidia vijana kutimiza ndoto zao
Vijana wafanyao kazi kwenye boti ya Uto ni Yalo wakiandaa kung’oa nanga kwenye mji mkuu Suva nchini Fiji ili kusambaza vifaa vya misaada kufuatia kimbunga kilichopiga nchi hiyo mwaka 2018. Picha | Uto ni Yalo Trust/Samuela Ulacake.
- Ni pamoja na kuwashirikisha katika shughuli za maendeleo na uongozi.
- Usawa wa kijinsia na kutoa fursa sawa kwa vijana kwasisitizwa.
Dar es salaam. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Antonio Guterres ameitaka jamii kuwasaidia vijana kwa kuwekeza kwenye kuwapatia elimu na kuwajengea uwezo wa kiujuzi kupitia mikutano pamoja na kufanya mabadiliko katika mifumo ya elimu.
Kwa mujibu wa UN, vijana wenye chini ya umri wa miaka 30 ni nusu ya wakazi wote duniani na idadi inatarajiwa kufikia asilimia 57 ifikapo mwishoni mwa mwaka 2030.
Guteress katika ujumbe wake wa Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Vijana jana Agosti 12, 2022 amesema jamii inapaswa kuunga mkono usawa wa kijinsia na fursa zinazotolewa zihakikishe zinawashirikisha vijana iwe ni maisha ya kiraia au hata yale ya kisiasa.
“Haitoshi kuwasikiliza tu vijana, tunahitaji kuwajumuisha katika mifumo ya kufanya maamuzi katika ngazi za ndani, kitaifa kwa kimataifa,” amesema Guterres
Siku ya kimataifa ya vijana huadhimishwa na nchi wanachama wa UN kila ifikapo Agosti 12 kila mwaka huku dhumuni kuu ikiwa ni kutambua mchango wa vijana katika kuhamasisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya vijana mwaka huu kwa Tanzania yaliongozwa na Kaulimbiu isemayo ”Kila mmoja anahusika kujenga uchumi imara,ustawi na maendeleo endelevu, Jiandae kuhesabiwa”
Katika kuweka msisitizo katika kauli mbiu ya mwaka huu, Guterres amesema vizazi vyote vinapaswa kuungana ili kuvunja vizuizi na kufanya kazi kwa pamoja.
“Ubaguzi wa umri, upendeleo na ubaguzi mwingine wa aina yoyote ambao unawatupa nje vijana kwenye maeneo ya kufanya maamuzi kuhusu maisha yao unapaswa kuondolewa,” amesema Guterres.
Latest