Zaidi ya Sh22 bilioni kuimarisha afya ya mimea, usalama wa chakula Tanzania
- Zitatolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) kwa kushirikiana na Muungano wa Ulaya (EU).
- Zitasaidia kufungua soko la kimataifa kwa bidhaa za Tanzania.
- Ndege zisizo na rubani kutumika katika mradi huo.
Katika kutekeleza lengo namba 15 la Maendeleo Endelevu (SDGs) kuhusu kuimarisha uhai wa viumbe vya nchi kavu, Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) kwa kushirikiana na Muungano wa Ulaya (EU) limezindua mradi wa kuimarisha huduma za afya ya mimea na usalama wa chakula nchini Tanzania.
Afisa Afya ya Mimea kutoka FAO, Mushobozi Baithani amesema lengo la mradi huo ni kuboresha sekta ya mimea na mazao pamoja na kutatua changamoto kwa wafanyabiashara.
“Tanzania wakulima wake wamekuwa wakilima mazao na kusafirisha nje ya nchi lakini zimetokea changamoto kwamba mzigo unafika kule halafu unazuiwa kuingia pengine baada ya kukaguliwa unakutwa na visumbufu, wadudu au umepimwa wamekuta viwango vya viautilifu vilivyowekwa kwenye chakula ni vingi na hakifai kuliwa,” amesema Baithani.
Soma zaidi:
- Maumivu yalivyochochea wanakijiji kutunza miundombinu ya maji Simiyu
-
Mikutano ilivyowazimisha viongozi wa ‘wasusa, twala’ Tanga
-
Vita mbichi: Wakazi wa Pangani wanavyohamasishana kupata chanjo ya Uviko-19
Amesema mradi huo wa miaka mitatu na utatumia zaidi ya Dola za Marekani milioni 9 sawa na Sh22 bilioni.
“Umoja wa Ulaya umetoa zaidi ya Dola za Marekani milioni 9 ambazo tutaenda kurekebisha vituo 19 mipakani, tutarekebisha maabara nne, tutanunua vifaaa pamoja na kutengeneza mfumo wa kidigitali utakaotumika kukusanya takwimu mashambani na tumetoa ufadhili wa masomo ya urushaji wa ndege zisizo na rubani kwa wakaguzi 20,” ameongeza Baithani.
Efraim Njau ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Udhibiti wa Viuatilifu Tanzania (TPHPA) amesema mradi huo utatusaidia kufungua masoko mapya ya kimataifa ikizingatiwa kuwa utawawezesha wakulima kuzalisha mazao yenye ubora wa hali ya juu.
“Tutaenda kulima mazao mapya kama soko la maparachihi, maua, pilipili na tangawizi sasa mazao haya yanafuata huu mfumo,” amesema Njau.
Mradi huo pia utatoa mafunzo ya kuendesha ndege zisizo na rubani kwa wakaguzi 20 ili kuwawezesha kufanya tafiti na uchunguzi wa visumbufu kama wadudu na magonjwa yanayoshambulia mazao ya chakula, biashara pamoja na mimea.