Mtandao wa barabara utakavyoboresha maisha Mwanza
Mwonekano wa Barabara zilizotengenezwa kwa fedha za mfuko wa jimbo katika Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza. Picha | Mariam John.
- Ni kilomita 126 zilizojengwa wilayani Ilemela.
- Zitarahisisha usafiri wa bidhaa na abiria.
Mwanza. Jumla ya kilometa 126 za mtandao wa barabara zinazounganisha kata na Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza zimefunguliwa kupitia fedha za mfuko wa jimbo.
Barabara hizo za molamu, zimefunguliwa chini ya Usimamizi wa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (Tarura)
Mratibu wa barabara kutoka ofisi ya Mbunge wa jimbo Hilo, Mpunzi Mbegeje amesema ufunguaji na uunganishaji wa mtandao huo wa barabara utasaidia wananchi kuwa na uhakika wa usafiri wakati wote na pia utasaidia kuendesha shughuli zao za kiuchumi na kijamii za kila siku.
“Tunatambua changamoto za uharibifu wa barabara hasa kipindi cha mvua, hivyo mfuko wa jimbo umetekeleza ahadi yake kwa wananchi katika uchaguzi uliopita kuwa zingetengenezwa ili kuondoa changamoto zilizokuwepo,” amesema Mbegeje.
Mratibu hiyo ameiomba Serikali kuongeza bajeti ya fedha za mfuko wa jimbo na bajeti ya Tarura ya Ilemela ili kukidhi mahitaji ya wananchi ukilinganisha na uhitaji kwa kuwa wilaya hiyo imekuwa ikikua kwa kasi siku hadi siku hali inayosababisha mbunge kutoa fedha zake mfukoni kugharamia ukarabati wa barabara hizo.
Awali Msimamizi wa mtandao huo wa barabara kutoka Tarura Mhandisi Said Irema amesema ofisi yake imeshapokea barabara 47 zilizofunguliwa kwa ajili ya kuzihudumia kama mamlaka ya usimamizi wa barabara ndani ya wilaya hiyo.
“Tunamshukuru kwa ukarabati huu sasa kazi zitarahisisha katika kusafirisha bidhaa na huduma nyingine za kijamii,” amesema Rubanila Matoforo.
Barabara zilizofunguliwa ni pamoja na Buswelu – Mbogamboga, Kahama senta- Isela, Isela – Zahanati ya Kahama na Nyamandoke- Nyamhongolo.