Biteko aagiza tozo za madini kwa wachimbaji wadogo zipitiwe upya
- Ni zile zinazotozwa na halmashauri ambazo zinawaumiza wachimbaji.
- Awataka wachimbaji waache kulalamika.
Mwanza. Serikali imeziagiza halmashauri zote nchini kuangalia upya mrundikano wa tozo kwenye sekta ya madini hususani kwa wachimbaji wadogo ili zipunguze usumbufu wa namna ya kuzilipa.
Agizo hilo limetolewa leo Oktoba 11 na Waziri wa madini Dotto Biteko leo wakati akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini pamoja na wanunuzi wa dhahabu mkoani Mwanza ambao moja ya changamoto walizoziainisha ni pamoja na mrundikano wa tozo kwenye maeneo yao ya uchimbaji.
Kutokana na changamoto hiyo Waziri Biteko amesema pamoja na kwamba tozo hizo ni moja ya makusanyo ya mapato ya halmashauri lakini halmashauri zingine zimezidi kwa kuwa zinakusanya tozo hizo bila kuzipitisha kwenye sheria ndogo za halmashauri.
“Mchimbaji huyo anatozwa tozo kila sehemu, kwenye mawe kuna tozo, kwenye karasha, na sijui kwenye mifuko ya udongo tozo, mchimbaji kama huyu ukimtoza kila mahali utamchanganya hata kama ni ndogo, niagize halmashauri zitengeneze utaratibu wa tozo na ufanane nchi nzima ili kumpa unafuu mchimbaji kufanya shughuli zake kwa amani,” amesema Biteko
Mbali na hilo pia Waziri amewatoa hofu wachimbaji hao kuwa atashirikiana na wizara zingine katika kuwafikishia huduma muhimu kama maji, umeme pamoja na utengenezaji wa barabara.
Amesema mgodi wowote ambao haujapata umeme waandike mahitaji yao ili awasiliane na waziri wa nishati kwa ajili ya kuwapelekea huduma hiyo huku akiwataka kuacha kulalamika.
“Muache kulalamika nyinyi ni mabilionea wa kesho mnalalamikia kulipa bili kubwa za maji kwa Sh2000 kwa uniti wakati mwananchi wa kawaida hapo Sengerema analipia uniti hiyo kwa Sh1400 na wakati hana anachozalisha nyinyi mnalalamikia nini?,” amehoji Biteko
Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha mchimbaji na mnunuzi wa madini anafanya shughuli zake bila kikwazo na kwamba wizara hiyo iko mbioni kuanzisha viwanda vingine vikubwa vitatu vya kusafisha madini.
“Sisemi ni lini lakini huko mbeleni hatutaruhusu madini kwenda kusafishwa nje ya nchini wakati yanazalishwa hapa nchini, na mimi kama waziri mwenye dhamana sitaruhu hili litokee dhahabu itasafishwa nchini ndipo isafirishwe,” amesema Biteko.
Awali mwenyekiti wa chama cha wachimbaji wadogo wa dhahabu cha Mwerema, Richard Seni amesema tozo za halamshauri ni kubwa kuzidi mrahaba na mbaya zaidi zinatozwa kwenye malighafi.
“Chama kinapendekeza kuondolewa tozo zote zinazokinzana na sheria ya madini na ibaki asilimia 0.3 pekee ambayo nayo itozwe kwenye madini,” amesema Seni.