Tanzania yazungumza na taasisi za kifedha za kimataifa misamaha ya madeni
- Rais Samia aeleza kuwa Serikali inaendelea inaendelea mazungumzo na taasisi hizo kwa ajili ya kuomba kusamehewa madeni au kuwekewa ahueni katika urejeshaji
Mwanza. Serikali imesema inaendelea na mazungumzo na taasisi za kifedha za kimataifa kwa ajili ya kuomba kusamehewa madeni au kuwekewa ahueni katika urejeshaji wake ikiwa ni moja ya hatua za kuendelea kuimarisha uchumi baada ya janga la Uviko-19.
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameeleza jijini Dodoma leo kuwa mbali na hatua hiyo, watazungumza na taasisi za kifedha ili iweze kupata mikopo itakayosaidia kulipa madeni na kuhakikisha utekelezaji wa bajeti ya Serikali.
Rais Samia amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na Uviko-19 ikiwemo kuokoa maisha ya watu kwa kutoa chanjo ya maradhi hayo yanayoendelea kuitesa dunia na kutekeleza sera mbalimbali za kifedha na kiuchumi.
“Pamoja na hatua alizozieleza (Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania), tumehangaika kwenye taasisi za kifedha za kimataifa kuomba misamaha ya madeni au kurefushwa kwa madeni ili tulipe polepole na ikiwezekana watusamehe,” amesema Rais Samia wakati akifungua mkutano wa 20 wa taasisi za fedha ulioandaliwa na Benki kuu ya Tanzania (BOT).
“Sasa Serikali bado tunaendelea kuzungumza na taasisi hizo za kimataifa,” amesema Rais Samia.
Rais Samia Suluhu Hassan akifungua Mkutano wa 20 wa Taasisi za Fedha nchini wenye lengo la kupitia na kutatua changamoto mbalimbali katika sekta hiyo Novemba 25, 2021. Picha|Ikulu.
Mbali na hatua hiyo, amesema Serikali iliomba fedha zitakazopunguza makali ya athari za Uviko-19 ambazo walizipata na zinaendelea kusaidia taifa.
“Lakini pia kuna taasisi tutakazozungumza nazo humu ndani ili kuweza kupata fedha zaidi za kuweza kulipia madeni yetu na ‘kubalance’ (kukamilisha) bajeti yetu,” amesema.
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo hazikuzuia watu wake kutoka nje ikiwa ni moja ya njia za kupunguza makali ya athari za Uviko-19 katika shughuli za kijamii na kiuchumi.
Tofauti na miaka miwili iliyopita, mwaka 2020 uchumi ulikua kwa wastani wa asilimia 4.8 kiwango ambacho ni cha chini ya wastani wa asilimia 7 iliyorekodiwa mwaka 2019 kutokana na athari za Uviko-19, kwa mujibu wa BoT.
“Ni matarajio yetu kuwa uchumi wa Tanzania utakuwa kwa kasi na kufikia kasi ya zaidi 8% katika miaka mitano ijayo. Makadirio haya yanatokana na kuongezeka kwa matumizi ya rasilimali na ongezeko la tija katika shughuli za uzalishaji,” amesema Prof Florens Luoga, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania.
Makala hii imefadhiliwa na Shirika la maendeleo ya habari la International Media Support (IMS) na Umoja wa Ulaya (EU).
