Ombi la Rais Samia kwa Umoja wa Mataifa
Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza Septemba 23, 2021 alipokuwa akihutubia mkutano mkuu wa baraza la Umoja wa Mataifa (UN), Jijini New York, Marekani. Picha| Ikulu.
- Ni pamoja nchi zinazoendelea kupewa hakimiliki ya utengenezwaji wa chanjo ya Corona.
- Nchi zenye chanjo zisaidie nchi zisizo na afua hiyo ya Corona.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ameuomba Umoja wa Mataifa (UN) kuzipatia haki miliki ya utengenezaji wa chanjo ya Uviko-19 nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania ili kuongeza kasi ya mapambano dhidi ya janga la Corona duniani.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo, kwa sasa kasi ya usambazaji wa chanjo iko chini ikilinganishwa na kasi ya kusambaa kwa ugonjwa huo hasa katika nchi za Afrika.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza Septemba 23, 2021 alipokuwa akihutubia mkutano mkuu wa baraza la Umoja wa Mataifa (UN), Jijini New York, Marekani amesema endapo nchi zinazoendelea zingepatiwa hakimiliki ya uzalishaji wa chanjo, ingekuwa rahisi kuambana na Corona.
“Ombi letu ni kwamba hakimiliki ya kutengeneza chanjo ya Uviko-19 itolewe kwa nchi zinazoendelea ili tuweze kupambana na janga hili hatari, hii siyo tu hatua ya muhimu ya kumaliza janga hili lakini pia ni jambo sahihi litakalosaidia kuokoa ulimwengu mzima,” amesema Rais Samia.
Tangu kuripotiwa kwa janga la Uviko-19 mwishoni mwa mwaka 2019, limesababisha athari mbalimbali za kiuchumi na kijamii na hivyo kuzorotesha juhudi za kuleta maendeleo duniani.
Ugonjwa huo pia umepunguza kasi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ya mwaka 2030 katika muda uliopangwa katika baadhi ya nyanja huku taarifa zikionyesha kuwa kumekuwa na athari zilizorudisha nyuma mafanikio yaliyokwishapatikana.
Kwa mujibu wa Rais Samia, takriban watu milioni 71 duniani wanatarajiwa kurejea katika umasikini licha ya kwamba walikwishaondokana na hali hiyo. Ametilia msisitizo kuwa ipo haja ya kuunganisha juhudi za kubadili hali hiyo hasa kwa kuwa changamoto za janga la Corna hazijali hali ya nchi ilivyo.
Kwa Tanzania, Rais Samia amesema zimekuwepo juhudi za kupambana na Corona ikiwemo programu ya kutoa chanjo kwa watu nchi nzima.
“Hakuna aliye salama hadi wote tuwe salama, ni muhimu nchi zenye chanjo zisaidie nchi zisizo na chanjo ili kukabiliana na janga hili la Uviko-19,” amesema Rais Samia.
Pembeni ya mkutano huo, Rais Samia amekutana na viongozi mbalimbali wa nchi na taasisi za kimataifa akiwemo Rais wa Benki ya Dunia, David Malpass aliyekubali kuisaidia Tanzania kupata chanjo dhidi ya Uviko-19.
Latest
