Serikali yaingilia kati bei za vinywaji, vifaa vya ujenzi kupaa
- Yaagiza wazalishaji kushusha bei kwa sababu zimepanda kiholela
- Yasema hakuna sababu ya bei kupanda kwa sababu viwanda vinaweza kulisha zaidi.
- Kuwachukulia hatua waliopandisha bei hizo.
Dar es Salaam. Kufuatia malalamiko ya wananchi ya kupanda kwa bei za vifaa vya ujenzi na vinywaji ikiwemo soda katika baadhi ya maeneo nchini Tanzania, Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwemo kuwaagiza wazalishaji kushusha bei hizo ambazo inadai zimepanda kiholela.
Baadhi ya vifaa vilivyopanda bei ndani ya miezi michache iliyopita ni pamoja na saruji, nondo na vinywaji aina ya soda na juisi, jambo lililosababisha maumivu kwa wananchi wanaojenga na wafanyabiashara huku wengine wakisitisha ujenzi mpaka pale bei itakapotulia.
Kutokana na kadhia hiyo, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dk Ashatu Kijaji katika taarifa yake iliyotolewa leo Februari 7, 2022 amesema Serikali ilifanya uchunguzi kuhusu mwenendo wa uzalishaji na usambazaji wa vifaa vya ujenzi katika kipindi cha mwezi Novemba 2021 hadi mwezi Februari 2022 na kubaini mambo matano kuhusu bei hizo.
Dk Kijaji amesema ongezeko holela la bei za vifaa vya ujenzi, hususan saruji na nondo linasababishwa na wazalishaji wa bidhaa husika kufanya uzalishaji banifu na kutokuwa na mfumo wa wazi wa usambazaji wa bidhaa hizo ambapo kuna mnyororo mrefu wa usambazaji wa bidhaa kutoka kiwandani mpaka kumfikia mlaji wa mwisho.
“Gharama halisi za uzalishaji wa saruji haiakisiwi katika bei ya saruji iliyopo sokoni ikilinganishwa na uwiano huo katika nchi jirani na kwingineko duniani.
“Ongezeko la bei ya saruji na nondo halina uwiano halisi na gharama za usafirishaji na usambazaji,” amesema Dk Kijaji.
Amesema pia kuwa bei ya saruji iliyopo sokoni haina uhusiano na mwenendo wa nguvu za utashi wa mlaji na ugavi (demand and supply forces).
“Kuna ucheleweshwaji wa makusudi wa utoaji wa saruji kutoka viwandani kwenda kwa wasambazaji (distributors) na wanunuzi wa ndani, hususan wale wadogo, waliokwishalipia saruji husika tofauti na wanunuzi wa nje ambao hupatiwa saruji kwa urahisi zaidi,” amesema Kijaji katika taarifa yake.
Pamoja na mambo mengine, hali hiyo imesebabisha wasambazaji hao kupandisha bei za saruji ili kufidia gharama zilizotumika kuchukua mzigo.
Serikali haitavumilia tabia ya wafanyabiashara wachache kuanzia wazalishaji hadi wasambazaji wenye dhamira ovu ya kuwaumiza wananchi kwa kujiamulia kupandisha bei za bidhaa bila kufuata utaratibu kwa manufaa yao binafsi. Picha| Mtandao.Atoa maagizo mazito
Kufuatia uchunguzi huo, Serikali imedai bei zimepanda kiholela bila utaratibu na hivyo wazalishaji, wasambazaji na wafanyabishara wa vifaa vya ujenzi wanatakiwa kushusha mara moja bei za bidhaa hizo walizopandisha kiholela na kuuza bidhaa hizo kwa kuzingatia gharama halisi za uzalishaji na usambazaji.
“Agizo hili linahusu pia bei za vinywaji baridi,” amesema Dk Kijaji na kuzielekeza mamlaka zote za udhibiti kuchukua hatua kali dhidi ya walimbikizaji na wauzaji kupitia mlango wa nyuma (black market) wanaosababisha bei za bidhaa kupanda sokoni, ili kuhakikisha kuwa bidhaa zinafika sokoni kwa wakati na kwa bei shindani.
Kwa kuwa kitendo cha kupanga bei kati ya washindani ni uhujumu uchumi, amezielekeza mamlaka husika kuchukua hatua kali dhidi ya wote watakaobainika kupanga bei kwa bidhaa kwa mujibu wa sheria za Nchi huku akiwataka wazalishaji kuzalisha bidhaa hizo kulingana na uwezo wa viwanda uliosimikwa ili kukidhi mahitaji ya soko.
“Ninawaelekeza wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuweka mifumo mizuri ya usambazaji wa vifaa hivyo ili kuzuia kupanda kwa bei kunakoweza kuzuilika.
“ninawaelekeza Maafisa Biashara wa Mikoa kote nchini waendelee kufuatilia kwa karibu mwenendo wa bei za bidhaa mbalimbali kwenye maeneo yao na kuwasilisha taarifa hizo mara kwa mara Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, kupitia Ofisi za Makatibu Tawala wa Mikoa, ili itakapobidi hatua stahiki zichukuliwe kwa wakati,” amesema Dk Kijaji.
Zinazohusiana:
- Kwanini ufuatilie mjadala wa bei ya korosho?
- Uzalishaji, mauzo bidhaa za viwandani vyapaa
- DPP aingilia kati sakata la uhaba wa saruji Tanzania
Mwenendo wa vifaa vya ujenzi
Kwa mujibu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, kwa sasa Tanzania ina viwanda 17 vya saruji vyenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya saruji hapa nchini.
Hata hivyo, matokeo ya uchunguzi yamebainisha kuwa viwanda vya saruji nchini vinazalisha kwa takribani asilimia 58 tu ya uwezo uliosimikwa wa viwanda hivyo.
“Hii inaashiria kuwa bado viwanda vya ndani vina uwezo wa kuongeza uzalishaji wa saruji ili kukidhi mahitaji ya ndani ya Nchi na kuweka bei shindani ya saruji sokoni,” amesema Dk Kijaji.
Kwa upande wa nondo, Tanzania ina viwanda 16 vinavyozalisha nondo vyenye uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.1 za ukubwa mbalimbali.
Hata hivyo, uchunguzi wa wizara hiyo umeonesha kuwa uzalishaji wa nondo viwandani kwa sasa hauzidi tani 750,000 pekee.
Kwa mujibu wa tathmini iliyofanywa na Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na FCC juu ya uhaba wa vifaa vya ujenzi nchini na upandaji wa bei kiholela ilibainika kuwa ingawa nondo na bidhaa zinazotokana na chuma zinapatikana kwa uchache, bei zake zimeongezeka sana katika kipindi tajwa.
Kupanda kwa bei ya vifaa vya ujezi kumechangia kuongeza gharama za maisha kwa Mtanzania mmoja mmoja, lakini pia imeendelea kuathiri uchumi wa wa nchi kwa kuongeza gharama za ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya kitaifa kama vile madarasa, hospitali pamoja na miradi mingine ya kimkakati.