Tanzania iwekeze katika mabaraza ya ardhi yanayotembea
- Mabaraza hayo yataongeza kasi ya kutatua migogoro ya ardhi.
- Hadi sasa kuna mabaraza 80 kati ya mabaraza 139 yanayopaswa kuundwa kote nchini.
Dar es salaam. Serikali ya Tanzania imeshauriwa kuwekeza kwenye mabaraza ya ardhi yanayotembea (Mobile Land Tribunal) kuwafikia wananchi wengi kwenye vijiji na kata ili kuongeza kasi ya utatuzi wa migogoro ya ardhi.
Mabaraza hayo yanayotembea yanatajwa kuwa yatasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa mabaraza ya ardhi katika kila wilaya nchini.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Ardhi, Maliasili na Utalii Mbunge Ally Makoa ameiambia Serikali jijini Dodoma Mei 26, 2022 kuwa ili kutatua uhaba wa mabaraza ya ardhi na nyumba nchini ni vyema Serikali ikaja na mkakati wa mabaraza ya ardhi yanayotembea ili kuongeza kasi ya kutatua migogoro nchini.
“Serikali ihakikishe inaanzisha mabaraza haya katika kila wilaya nchini ili kusogeza huduma hiyo karibu na wananchi. Vile vile, Serikali iwekeze zaidi katika mabaraza yanayotembea (Mobile Land Tribunal) ili kuwafikia wananchi wengi kwenye vijiji na kata.” amesema Makoa.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ina jukumu la kuanzisha, kusimamia na kuhudumia mabaraza ya ardhi na nyumba ya wilaya kwa lengo la kutatua migogoro ya ardhi nchini.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula ameliambia bunge kuwa hadi sasa wizara imeshaunda mabaraza 80 kati ya mabaraza 139 yanayotakiwa kisheria ambayo yamekuwa yakipokea, kusikiliza na kuamua mashauri ya ardhi.
Katika mwaka 2022/23 inatarajia kushughulikia mashauri 33,250 na itawezesha Mabaraza mapya 59 kuanza kutoa huduma na hivyo kufanya mabaraza yanayotoa huduma katika wilaya zote nchini.
Soma zaidi:
- Mgogoro wa ardhi unavyosababisha wanafunzi 200 wabanane darasa moja Mbeya
- Kigoma kinara usajili mashamba Tanzania bara
Utatuzi wa migogoro ya ardhi kiutawala
Waziri Mabula amesema katika mwaka 2021/22 wizara ilipanga kutatua migogoro ya ardhi 1,000 kiutawala lakini kufikia Mei 15, 2022 migogoro 1,898 kati ya migogoro 1,635 iliyopokelewa ilikuwa imetatuliwa.
Wizara imeendelea kudhibiti migogoro ya ardhi kwa kutumia njia mbalimbali na kuhusisha wizara za kisekta na wadau wa sekta ya ardhi ikiwemo kutoa elimu kwa umma kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.”
“Tumeongeza kasi ya umilikishaji ardhi, kufanya utambuzi wa vipande vya ardhi kwenye maeneo yaliyoendelezwa, kuendelea kubadilisha nyaraka za upangaji na upimaji na umilikishaji ardhi kutoka analogia kuwa za kidigitali,
“Kuandaa na kusimamia mipango ya matumizi ya ardhi, kudhibiti uvamizi na kuchukua hatua za kisheria, kuwajengea uwezo watumishi ili kuimarisha utoaji huduma na kuimarisha utendaji wa madawati ya kushughulikia malalamiko katika Ofisi za Ardhi za Mikoa.” amesema Waziri Mabula.
Wabunge waingilia kati
Baadhi ya wabunge wamepongeza jitihada za wizara hiyo kwa kuendelea kutatua migogoro ya ardhi nchini ambayo imekuwa ni changamoto kwa wananchi.
“Kama kuna wizara ambayo imeweza kuitika wito wa Watanzania huhusu migogoro mbalimbali ni wizara hii ya ardhi……kwa mara ya kwanza nimeona mapendekezo machache sana ya watu wanaotaka kuongea kwenye wizara hii, kwasababu migogoro mingi imetatuliwa na serikali kupitia wizara hii,” amesema Mbunge wa Madaba, Joseph Mhagama.
Wizara ya ardhi imekuwa ikishughulikia migogoro ya ardhi nchini kupitia mabaraza yake ambayo yanaendelea kuundwa ili kutatua migogoro hiyo.