Shughuli za kibinadamu zatishia uhai Ziwa Victoria
- Shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo ni hatari kwa ziwa hilo.
- Zinatishia ghuba ya ziwa hilo lisipumue.
Dar es Salaam. Shirika la Usimamizi wa Mazingira na Maendeleo (EMEDO) limetahadharisha kuwa shughuli za kibinadamu zinazofanyika katika fukwe za Ziwa Victoria, zinatishia ghuba ya ziwa hilo iliyopo Luchelele jijini Mwanza na kwamba ikiwa hatua stahiki hazitachukuliwa mapema kuna hatari ya kutoweka.
Mkurugenzi wa shirika hilo, Edtrudith Lukanga amesema shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo katika ghuba hiyo ambayo husaidia ziwa kupumua ni hatari kwani zinasababisha kemikali za kilimo na udongo kuingia ziwani na kutishia kutoweka huku zikisababisha pia madhara kwa viumbe hai ikiwemo samaki.
Amesema Ziwa Victoria ni raslimali kubwa inayopaswa kulindwa na kila mmoja ambapo kwa upande wa shirika la EMEDO limekuwa likielimisha jamii katika utunzaji wa ziwa hilo hususani kutotupa ovyo taka za plastiki.
“Tuna kampeni ya kuhamasisha kila mmoja awajibike katika utunzaji wa mazingira ambapo katika mitaa 10 ya Kata ya Luchelele tumeanzisha vikundi vinavyopita kaya kwa kaya kutoa elimu na pia kukusanya taka na kuzipeleka katika vituo maalum tunawahimiza kuona taka kama rasilimali ambapo wenye mawazo ya ubunifu tunawawezesha kutengeneza bidhaa mbalimbali,” amesema Lukanga.
Pia Lukanga ameongeza kuwa shirika hilo limetoa mwongozo wa kuendeleza uvuvi mdogo ili kuhakikisha unakuwa endelevu kwa mstakabali wa chakula na kujikwamua kiuchumi huku pia wakiwasaidia wavuvi kuondokana na changamoto za kiusalama ziwani.
Baadhi ya wakazi jijini Mwanza wamesema wanashirikiana na shirika la EMEDO ili kuielimisha jamii kutambua umuhimu wa kutunza mazingira hususani Ziwa Victoria ili kuendelea kuilinda rasilimali hiyo muhimu nchini na duniani kwa ujumla.
“Kazi ya kutunza Ziwa Victoria ni ya kwetu sote tuna haki ya kulilinda na kulitunza hivyo kila mmoja ana wajibu kuhakikisha haliharibiwi na shughuli za kawaida za binadamu,” amesema Musa Tembe, mkazi wa Luchelele Mwanza.