Wizara ya Elimu yatangaza ufadhili diploma ya ualimu makundi maalumu
- Maombi yatapokelewa kwa siku 15 kuanzia Agosti 18 hadi 28, 2025.
- Wanufaika ni wanafunzi wa shahada ya elimu maalum.
Arusha. Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetangaza fursa ya ufadhili wa masomo ya elimu ya juu kwa ngazi stashahada ya ualimu wa elimu ya juu kwa miaka miwili.
Taarifa ya Prof.Carolyne Nombo, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo iliyotolewa Agosti 20, 2025 inabainisha kuwa maombi yatakayopokelewa kwa ajili ya ufadhili huo ni kwa wanachuo wanaosoma stashahada ya elimu maalumu katika maeneo ya ulemavu wa akili, usonji, uziwi, na ulemavu wa uoni.
Miongoni mwa sifa za msingi zilizoanishwa na Wizara hiyo ni kuwa Mtanzania pamoja na kudahiliwa chuo cha ualimu kinachotambulika na Serikali kinatoa Stashahada ya Ualimu Elimu Maalumu.
“Nakala za kuwasilisha ni barua ya kuomba ufadhili ikionesha kozi unayosoma, namba ya simu na barua pepe, nakala ya vyeti vya kitaaluma vilivyothibitishwa na mwanasheria, cheti cha kuzaliwa kilichothibitishwa na mwanasheria na barua kutoka kwa mkuu wa chuo ikionesha kuwa umedahiliwa katika chuo husika,” imebainisha taarifa ya Nombo.
Aidha, Wizara hiyo imebainisha kuwa ufadhili huo utahusisha mahitaji mbalimbali ikiwemo ada ya mafunzo miichango mingine ya chuo (kama ulinzi, ukarabati), vifaa vya kufundishia na kujifunzia, nauli na bima ya Afya.
Masharti ya ufadhili
Wizara ya Elimu imesema miongoni mwa masharti muhimu ya kupata ufadhili huo ni pamoja na kusoma, kuelewa na kusaini mkataba wa makubaliano ya ufadhili wa masomo kati yake na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na kuwa na akaunti ya benki kwa ajili ya fedha atakazolipwa moja kwa moja.
“Mnufaika hataruhusiwa kubadilisha programu ya masomo aliyopatia ufadhili bila idhini ya Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, mnufaika hataruhusiwa kuahirisha masomo, isipokuwa kwa sababu za kiafya, na kuthibitishwa na Daktari kutoka katika Kituo cha Afya au Hospitali inayotambuklika na Serikali,” imeongeza wizara hiyo.
Ikiwa mnufaika ataghairi fursa ya ufadhili, atapaswa kutoa taarifa kwa maandishi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia kwa Mkuu wa chuo alichodahiliwa na kujisajili.
Taarifa ya Nombo imebainisha kuwa maombi ya ufadhili huo yanatakiwa kuwasilishwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ndani ya siku 15 kuanzia Agosti 18 hadi 28, 2025.
Maombi hayo pia yanaweza kutumwa kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia sanduku la Posta S.L.P 10 Dodoma na rodha ya Wanachuo watakaokuwa wamepata ufadhili huo itawekwa katika tovuti ya Wizara (www.moe.go.tz).