Watumiaji wa Netflix waongezeka, kasi ya mtandao ikipungua
- Kati ya Aprili na Juni, mtandao huo umesajili watumiaji milioni 10.
- Mapato ya mtandao huo ni makubwa kurekodiwa yakilinganishwa na mwaka uliopita.
- Ongezeko hilo limesababisha kasi ya mtandao huo kupungua.
Dar es Salaam. Mtandao wa kuonyesha filamu mtandaoni wa Netflix umeonya kuwepo na changamoto ya kupungua kasi ya mtandao huo baada ya watumiaji wa mtandao huo kuongezeka maradufu.
Netflix ambayo imekuwa ni faraja kwa watu wengi hasa katika kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa Corona, imesema kati ya Aprili na Juni, watu wapya milioni 10 wamejisajili kwenye mtandao huo.
Kwa mujibu wa habari iliyotolewa na Shirika la Habari la Uingereza la BBC, mtandao huo kwa mwaka 2020 peke yake, umesajili watu milioni 26 ambao ni pungufu ya milioni mbili tu kuifikia idadi ya watu waliojisaliwa mwaka wa 2019.
“Netflix ilipata watumiaji wapya milioni 28 million kwa mwaka mzima wa 2019,” imesomeka sehemu ya habari ya BBC.
Ongezeko hilo limeenda sambamba na mapato ya kampuni hiyo ambapo Netflix imeripoti ongezeko la asilimia 25 katika mapato yake ikifikia Sh141.5 trilioni huku faida iliyopatikana ikiwa ni Sh 1.6 trilioni ongezeko kutoka Sh628 bilioni mwaka mmoja nyuma.
Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watumiaji hao, kasi ya mtandao huo imepungua katika kipindi hicho.
Zinazohusiana
- “Da 5 Bloods”: Filamu itakayokufundisha maana halisi ya uzalendo
- Jifunze nguvu ya familia katika filamu ya “Coffee and Kareem”
- Unatafuta filamu ya wikiendi? Confidential Spenser inakusubiri
Hata hivyo, wachambuzi mbalimbali wamesema huenda kasi ya watu kujisajili kwenye mtandao huo ikashuka baada ya nchi mbalimbali kuanza kulegeza masharti dhidi ya Corona na hivyo kuruhusu muingiliano na kuchangamana kwa watu.
Mtumiaji wa mtandao huo Alex Makundi wa jijini dar es Salaam amesema huenda akaungana na wale ambao watapunguza idadi ya waliojisajili kwenye mtandao huo kwani kwa sasa maisha yameanza kurudi kawaida.
“Mimi ninapenda kwenda kwenye kumbi za simema na rafiki zangu kuangalia filamu. Kuna skrini kubwa, viti na sauti iliyopangiliwa vizuri.
“Ugonjwa wa corona ulipoingia, kumbi hizo zilifungwa kwa kuwa napenda kuangalia filamu, nilijiunga na Netlix kwa sasa sina sababu ya kuendelea,” Amesema Makundi.