Wanaowanyanyapaa wenye VVU waonywa, Serikali ikihimiza usawa

December 1, 2021 12:47 pm · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Yasema vitendo, kauli au mitazamo ya unyanyapaa na ubaguzi kwa kundi hilo havikubaliki.
  • Watumishi wa afya nao waonywa kuvunjisha siri za Waviu.

Mwanza. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameziagiza mamlaka husika kuchukua hatua kali za kisheria kwa watu watakaobainika kuwanyanyapaa na kuwabagua watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi (Waviu).

Waziri Majaliwa amesema vitendo, kauli au mitazamo ya unyanyapaa na ubaguzi kwa kundi hilo havikubaliki.

Akizungumza kwenye maadhmisho ya Siku ya Ukimwi Duniani iliyofanyika kitaifa mkoani Mbeya leo Desemba 1, 2021, Majaliwa amesema yapo madai kuwa watumishi wa afya wana tabia za unyanyapaa na kuvujisha siri za Waviu wanapotoa huduma katika vituo vya tiba na matunzo.

“Ninaelewa kuwa unyanyapaa na ubaguzi kwa Waviu bado ni changamoto kubwa katika jamii zetu, vitendo na tabia hizi hazikubaliki ziripotiwe mara moja pindi vinapotokea,” amesema Majaliwa.

Kiongozi huyo amesema tabia hizo zinakwaza na kurudisha nyuma juhudi za mwitikio wa mapambano dhidi ya Ukimwi nchini na kuwa Waviu wanaona aibu kutumia huduma za VVU na Ukimwi zilizopo kwa sababu ya unyanyapaa na ubaguzi hasa maeneo ya vijijini.

Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani  mwaka huu yana kauli mbiu isemayo “Zingatia Usawa , Tokomeza Ukiwmi, Tokomeza Magonjwa ya Mlipuko”.

Mtendaji huyo mkuu wa nchi amesema ni kauli mbiu ambayo inazingatia usawa kwa kuwa Ukimwi hauchagui umri au rika.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza kwenye maadhmisho ya Siku ya Ukimwi Duniani iliyofanyika kitaifa mkoani Mbeya leo Desemba 1, 2021. Picha| Ofisi ya Waziri Mkuu.

Katika kutekeleza kauli mbiu hiyo kwa vitendo uwekezaji unatakiwa uzingatie mahitaji halisi kwa kila kundi, mazingira halisi na uhatarishi uliopo lakini pia kuzingatia haki za binadamu ili huduma zote zinazohusu masuala ya VVU na Ukimwi zitolewe kwa usawa unaohitajika.

Awali Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Utaribu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu, Jenista Mhagama  amesema huduma za  vidonge vya kufubaza makali ya Ukimwi (ARV) kwa watu wanaoishi na VVU zinaendelea kuimarishwa kwa kuhakikisha kuwa wanaogundulika kuishi na VVU wanapaswa kuanza kutumia dawa hizo mapema pamoja na kuzingatia ufuasi sahihi wa huduma hizo.

Mhagama amesema katika kudhibiti kuenea kwa maambukizi mapya ya VVU, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo inaendelea kutekeleza mkakati wa nne wa Taifa wa kudhibiti Ukimwi kwa kushirikisha sekta zote nchini.

Mkakati huo wa mwaka 2018/19 hadi 2020/23 umelenga kupunguza maambukizi mapya ya VVU na vifo vinavyohusiana na Ukimwi.

Mwenyekiti wa Baraza la Watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi Tanzania (NACOPHA) , Leticia Maurice amepongeza Serikali kwa jitihada zake za kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali nchini ikiwemo afya.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW