Waliougua kipindupindu Mwanza wafikia 34
- 21 waripotiwa wilayani Magu, 13 Ilemela.
- Elimu kwa umma, usafi binafsi na wa mazingira wasisitizwa.
Mwanza. Idadi ya watu walioripotiwa kuugua ugonjwa wa kipindupindu imefikia 34 jijini Mwanza ambapo 21 wameripotiwa katika Wilaya ya Magu na wengine wilayani Ilemela.
Awali watu saba ndio walioripotiwa kuwa na ugonjwa huo, huku wengine 18 wakiwekwa chini ya uangalizi maalum ili kubaini iwapo wana viashiria vya ugonjwa huo ulioingia jijini humo Januari 4, 2024.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Amos Makalla, aliyekuwa akizungumza katika kikao cha tahadhari ya ugonjwa wa kipindupindu amewaambia wajumbe wa kamati ya huduma za afya ya msingi leo Januari 10, 2024 kuanza mara moja kutekeleza mikakati ya kudhibiti ugonjwa huo ikiwemo kutoa elimu kwa umma hususan maeneo yenye mikusanyiko.
Soma zaidi : Saba waripotiwa kuugua kipindupindu Mwanza
Aidha, Mamlaka za maji ikiwemo Mwauwasa na Ruwasa zimetakiwa kuhakikisha wanatibu vizuri maji yanayotumika kwa wananchi huku Wakala wa barabara Mijini na Vijijini (Tarura) pamoja na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) wakitakiwa kuzibua mitaro ya maji kwa kuwa ni miongoni mwa vyanzo vinavyotunza uchafu unaosababisha vimelea vya ugonjwa huo.
“Mkasimamie maeneo yote ya vilabu vya pombe ya kienyeji ili visiwe chanzo cha maambukizi ya ugonjwa huo lakini pia suala la usafi wa mazingira kuanzia masokoni na sehemu zingine yapewe kipaumbele,” amesema Makalla.
Awali, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk Thomas Rutachunzibwa amesema wilaya zilizoathirika zaidi ni wilaya ya Magu yenye wagonjwa 21, pamoja na Ilemela yenye wagonjwa 13.
Hata hivyo, Dk. Tutachunzibwa amebainisha kuwa tayari wagonjwa wawili wamesharuhisiwa baada ya afya zao kuimarika.
Dalili za ugonjwa zatajwa
Kwa mujibu wa Dk. Rutachunzibwa dalili za ugonjwa wa kipindupindu huanza kuonekana kuanzia siku ya kwanza hadi ya tatu toka mtu ameze kimelea cha ugonjwa wa kipindupindu.
“Miongoni mwa dalili zinazojitokeza ni pamoja na kutapika na kuhara kama dalili kuu zingine ni misuli kulegea, na macho kuingia ndani,” amesema Dk.Rutachunzibwa
Soma zaidi : Ugonjwa wa kipindupindu waripotiwa Kagera, wanne wafariki
Kwa upande wake Danstan Ngenzi, Afisa ufuatiliaji na udhibiti wa magonjwa kutoka Wizara ya Afya, amebainisha kuwa pamoja na mikakati ya kudhibiti ugonjwa huo, jamii na makundi mengine ikiwemo ya usafirishaji na waganga wa tiba asili wanazingatiwa kuhakikisha wanapatiwa elimu ya kujikinga na ugonjwa huo.
Hii si mara ya kwanza ugonjwa wa kipindupindu kuripotiwa nchini Tanzania, hususan Kanda ya Ziwa, Disemba 4 2023, Mkuu wa Mkoa wa Kagera Fatma Mwasa alitangaza watu wanne kufariki kuutokana na ugonjwa huo huku wengine 18 wakichukuliwa sampuli kwa vipimo zaidi.