Wakulima wapewa siri kuongeza uzalishaji wa mazao Tanzania

April 25, 2023 7:28 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Washauriwa kutumia mbegu bora zilizofanyiwa utafiti.
  • ASA yasema mbegu hizo zina tija katika sekta ya kilimo.

Dar es Salaam. Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) umesisitiza wakulima kuendelea kutumia mbegu bora za mazao ambazo zimefanyiwa utafiti kulingana na mazingira ya sasa ili kuongeza tija katika kilimo na kulinda usalama wa chakula.

Msisitizo huo umetolewa hivi karibuni wilayani Kilosa mkoani Morogoro na Mtendaji Mkuu wa ASA, Sophia Kashenge huku akifafanua kuwa usalama wa nchi yoyote ni usalama wa chakula na haiwezekani kuwa na usalama wa chakula bila kuwa na usalama wa mbegu.

“Matumizi ya mbegu bora nchini bado yako chini, tunawasisitiza wananchi kuwa matumizi ya mbegu bora ni muhimu kwa sababu uchumi wowote katika kilimo unaanza na mbegu sahihi na bora, unapokuwa na mbegu bora tayari umeshajihakikishia asilimia 30 ya ongezekezo la kipato hivyo ukiongeza mbolea, mbinu bora za uzalishaji utavuna kwa tija,” amesema Dk Kashenge.

Ameeleza kuwa ASA imesimamia usalama wa chakula kwa kuzalisha mbegu bora za mazao mbalimbali pamoja na kuwa na wigo mpana wa kufanya kazi kutegemea na mipango ya Serikali.

Muonekano wa moja ya Shamba la mbegu za kilimo lililopo wilayani Kilosa mkoani Morogoro ambalo linamilikiwa na Wakala wa Mbegu za Kilimo nchini (ASA). Picha | ASA.

Uzalishaji wa mbegu uko hivi

Mashamba ya ASA yanayotumika kuzalishia mbegu yapo katika ikolojia zote za uzalishaji na yapo katika mikoa ya Arusha, Tanga, Pwani, Morogoro, Tabora, Kigoma, Songwe, Ruvuma na Iringa.

Katika msimu huu wa kilimo, ASA inatarajia kuzalisha tani 4,000 za mbegu baada ya ongezeko la bajeti ya wakala huo ya mwaka wa fedha 2022/23 kufikia Sh47 bilioni.

Wakala huo unafanya kazi kwa kupitia mashamba ya Serikali ambayo mpaka sasa yapo mashamba 16 na kati ya hayo, mashamba 13 yanafanya kazi na mengine matatu bado hayajakamilishwa umiliki wake huku yote yakiwa na jumla ya hekta 20,000.

Mwaka wa fedha 2017/18, ASA ilipata bajeti ya Sh1 bilioni ambayo iliwezesha kuzalisha  tani 500 tu za mbegu lakini 2021/22 Serikali ilitoa Sh10 bilioni na kuwezesha ASA kuzalisha tani 3,200 za mbegu.

Kupitia ongezeko la bajeti, ASA imeweza kufungua mashamba pori na kuongeza mashamba mapya ili kuendelea kupunguza ongezeko la mahitaji ya mbegu nchini.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW