Utoaji mikataba ya kazi waongezeka kwa asilimia 5.6 Tanzania

November 17, 2022 6:05 am · admin
Share
Tweet
Copy Link
  • Utoaji wa mikataba kwa wafanyakazi umeongezeka kutoka asilimia 59 mwaka 2020/21 mpaka 64.6 mwaka 2021/22.
  • Mkoa wa Kilimanjaro kinara utoaji mikataba, Mara yashika mkia.
  • Wanaume wanaopewa mikataba ni wengi kuliko wanawake. 

Dar es salaam. Huenda haki za wafanyakazi katika maeneo mbalimbali nchini zikaboreshwa zaidi siku zijazo, baada ya ripoti mpya kuonyesha kuwa utoaji wa mikataba ya ajira umeongezeka kwa asilimia 5.6 ndani ya mwaka mmoja. 

Ripoti ya Haki za Binadamu na Biashara ya mwaka 2022 iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Septemba 30 mwaka huu imeeleza kuwa utoaji wa mikataba kwa wafanyakazi umeongezeka kutoka asilimia 59 mwaka 2020/21 mpaka 64.6 mwaka 2021/22

“Utafiti uligundua kulikuwa na uboreshaji wa jumla katika suala utoaji wa mikataba ya ajira. Asilimia 64.6 ya wafanyakazi ambao walijibu utafiti huu walisema walikuwa na mikataba ya ajira, ongezeko asilimia 5.6 ikilinganishwa na utafiti wa awali uliofanyika mwaka 2020/21,’ inasomeka sehemu ya utafiti huo.

Kwa mujibu wa Chama Cha Wanasheria Tanzania (TLS) mkataba halali ni ule uliojengwa katika nguzo kuu tano ambazo ni makubaliano, hiari ya kuingia mkataba, malipo halali, uwezo wa kuingia mkataba pamoja na uhalali wa shughuli yenyewe itakayofanyika.


Soma zaidi


Katika ripoti hiyo ya LHRC imeonyesha Mkoa wa Kilimanjaro ndiyo unaoongoza kwa kutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi kwa asilimia 90, wakifuatiwa na Mwanza kwa asilimia 87, Geita (asilimia 86) na Dar es salaam kwa asilimia 81.

Licha ya ongezeko hilo baadhi ya mikoa nchini imeripotiwa kuwa na kiwango kidogo cha utoaji wa mikataba kwa waajiriwa cha chini ya asilimia 60 ukiwemo Mkoa wa Tanga wenye asilimia 59.

Mikoa mingine ni Dodoma kwa asilimia 53, Mtwara (asilimia 52) huku mkoa wa Mara ukiwa na kiwango cha chini zaidi cha asilimia 30.

Kwa mujibu wa utafiti huo idadi ya wafanyakazi wanaume waliopewa mikataba ya ajira ni kubwa wakiwa na asilimia 67 dhidi ya wanawake wenye asilimia 61.

Wafanyakazi nchini wamekuwa wakikabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo kutolipwa stahiki zao kwa wakati, kuachishwa kazi kiholela au kupangiwa majukumu ambayo hawakuridhia kutokana na kutokuwa na mikataba ya ajira.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW